WAZIRI wa Fedha na Mipango nchini Tanzania, Dk. Mwigulu Nchemba amesema, hadi kufikia Aprili 2021, malipo ya mafao na pensheni kwa wastani wa wastaafu 57,351 kila mwezi yamelipwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Pia, mirathi kwa warithi 1,187, malipo ya malezi kwa walezi 1,035 na malipo ya kiinua mgongo kwa watumishi wa Serikali walio kwenye mikataba 482.
Dk. Mwigulu, amesema hay oleo Jumatatu, tarehe 7 Juni 2021, bungeni jijini Dodoma, wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa mwaka 2021/22.
Amesema, wizara hiyo imeendelea kusimamia mafao na pensheni kwa watumishi wa Serikali ambao siyo wanachama wa mifuko ya hifadhi ya jamii pamoja na mirathi na malipo ya kiinua mgongo kwa watumishi wa Serikali walio katika mikataba na viongozi wa kisiasa.
“Aidha, Wizara inaendelea kufanya uhakiki wa wastaafu wote Tanzania nzima wanaopata malipo ya pensheni kupitia Hazina,” amesema Dk. Mwigulu
Waziri huyo amesema, mwaka 2020/21, wizara ilipanga kukusanya Sh.973.02 bilioni kutoka kwenye vyanzo mbalimbali ikiwemo gawio, michango kutoka taasisi na mashirika ya umma, marejesho ya mikopo, kodi za pango, mauzo ya leseni za udalali na nyaraka za zabuni.
“Hadi Aprili 2021, wamekusanya Sh.533.18 bilioni sawa na asilimia 54.7,” amesema Dk. Mwigulu
Leave a comment