SERIKALI ya Tanzania, imepanga kuboresha vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu, kwa kukarabati na kujenga miundombinu mipya pamoja na kuongeza vifaa vya kisasa vya kufundishia na kujifunzia. Anaripoti Nasra Bakari, DMC … (endelea)
Kauli hiyo imetolewa leo Ijumaa, tarehe 7 Mei 2021, bungeni jijini Dodoma, na naibu waziri wa elimu, sayansi na teknolojia, Omary Kipanga, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Thea Ntara.
Thea ameuliza, “je, Serikali ina mpango gani wa kujenga chuo kikuu cha Taifa Kusini mwa Tanzania na Kanda nyingine ambazo hazina vyuo vikuu.”
Akijibu swali hilo, Kipanga amesema, taratibu za uazishwaji wa vyuo vikuu vya umma, hazilengi kuanzisha vyuo vikuu vya kikanda, kimkoa au kiwilaya.
Amesema, vyuo vikuu vilivyopo nchini, vikiwemo vya serikali na binafsi, vinapokea wanafunzi kutoka kanda zote Tanzania Bara na visiwani na kutoka nje ya nchi na huu ndiyo utamaduni wa vyuo vikuu duniani kote
“Katika Kanda ya Kusini, kuna vituo vitatu vya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) vilivyopo katika makao makuu ya mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma,” amesema Kipanga.
“Aidha, kipo Chuo Kikuu cha Stella Maris (STeMMUCO), kilichopo Mkoa wa Mtwara na Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), kampasi ya Mtwara,” amesema.
Kipanga amesema, wanafanya hivyo ili kuongeza nafasi za udahili na ubora wa elimu itolewayo na hivyo kukidhi mahitaji ya nchi.
Leave a comment