SERIKALI ya Tanzania, imenunua vifaa vya kisasa vya mafunzo ya ukalimani kwa vitendo na matumizi ya tehama katika ukuzaji wa Lugha ya Kiswahili. Anaripoti Nasra Bakari, DMC … (endelea).
Hayo yamesemwa leo Ijumaa, tarehe 7 Mei 2021, bungeni jijini Dodoma, Naibu waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Pauline Gekul, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Singida Mjini (CCM), Mussa Sima.
“Je, Serikali ina mpango gani wa kuifanya Lugha ya Kiswahili kuwa bidhaa ya Kimataifa ili kuendeleza na kukuza utamaduni wetu duniani,” amehoji Sima.
Akijibu swali hilo, Gekul amesema, Serikali imeanzisha mipango ya kimkakati ya kukifanya Kiswahili kuwa bidhaa ya Kimataifa na tayari Kanzidata ya wataalamu wa Kiswahili imeanzishwa na wataalam 1,308 wamesajiliwa.
Amesema, Serikali tayari ina mpango wa kufundisha Kiswahili kwa wageni kupitia Balozi wa nje ya nchi.
“Vilevile, Serikali imeboresha na kuimarisha mafunzo stadi ya kufundisha Kiswahili kwa wageni pamoja na kutoa machapisho ya Kiswahili rahisi kwa wataalam.”
“Na pia ni kwa lengo la kusaidia nchi zilizoonesha nia ya kuingiza Kiswahili katika mitaala yao ya Elimu mfano Afrika Kusini, Namibia, Rwanda na Burundi,” amesema Gekul
Gekul amesema, mwaka 2019, wakati wa mkutano wa 39 wa wakuu na viongozi wa serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Africa (SADC), Serikali ilifanikiwa kukifanya Kiswahili kuwa moja ya lugha nne rasmi zinazotumiwa wakati wa vikao vya mikutano ya nchi hizo. Baadhi ya lugha zingine ni Kiingereza na Kifaransa.
Leave a comment