Wednesday , 8 May 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Prof. Kabudi avunja ukimya sakata Masheikh wa Uamsho
Habari za SiasaTangulizi

Prof. Kabudi avunja ukimya sakata Masheikh wa Uamsho

Wafuasi kundi la Uamsho
Spread the love

 

PROFESA Palamagamba Kabudi, Waziri wa Katiba na Sheria, amewataka Watanzania kutoingilia kati sakata la Masheikh 23 wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar, kwa kuwa liko mahakamani. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).

Waziri huyo wa Katiba na Sheria ametoa kauli hiyo leo Jumatano tarehe 28 Aprili 2021, bungeni jijini Dodoma.

Akizungumzia sakata hilo, Prof. Kabudi amesema, ushahidi wa kesi ya jinai Na. 121/2021 inayowakabili Masheikh hao katika Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, umekamilika, hivyo wananchi wanapaswa kusubiri uamuzi wa mahakama.

“Sasa ushahidi umekamilika, kesi iko mahakama kuu. Tuiachie mahakama kuu itoe uamuzi wake na asiyeridhika na maamuzi yatakayotolewa na mahakama, akate rufaa katika Mahakama ya Rufani ambayo ni ya muungano,” amesema Prof. Kabudi.

Prof. Kabudi amesema, kesi hiyo ilihamishiwa kutoka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwenda Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, baada ya upelelezi wake kukamilika.

“Shauri ambalo liko mahakamani na linaendelea ni shauri la masheikh wa uamsho, mnamo tarehe 15 Septemba 2020, shauri la jinai 21/2014 lililokuwepo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu lilifunguliwa rasmi katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, mara baada ya upelelezi kukamilika,” amesema Prof. Kabudi.

Prof. Kabudi amesema, usikilizwaji wa kesi hiyo ulipaswa kuanza tarehe 25 Machi 2021, ulikwama kufuatia kifo cha aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Dk. John Magufuli, kilichotokea tarehe 17 Machi mwaka huu, kwenye Hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam.

“Tarehe 17 Septemba 2020 mchakato wa kuhamisha kesi husika katika mahakama kuu ulikamilika, kesi hiyo ilikuwa ianze kusikilizwa tarehe 25 Machi 2021, lakini kutokana na msiba uliotupata ilisogezwa mbele hadi mwanzoni mwa mwezi Aprili, kwa sasa mahakama kuu imeanza kusikiliza kesi hiyo 121/2021 kuanzia tarehe 12 Aprili 2021.”

Prof. Palamagamba Kabudi, Waziri wa Katiba na Sheria

Masheikh hao waliakamtwa mwaka 2012 kisiwani Unguja, Zanzibar, kwa tuhuma za kuchochea vurugu.

Kauli hiyo ya Prof. Kabudi imetolewa baada ya mjadala wa sakata hilo kuibuka bungeni hivi karibuni, ambapo baadhi ya wabunge walihoji kwa nini mwenendo wa kesi hiyo unasua sua.

Miongoni mwa wabunge waliohoji hayo, ni Mbunge wa Kawe (CCM),Askofu Josephat Gwajima na Mbunge wa Chonga, Salum Mohammed Shafi.

Akichangia katika mjadala wa Mkadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka wa fedha 2021/2022, Shafi alihoji kwa nini kesi hiyo haikusikilizwa katika Mahakama Kuu ya Zanzibar, badala ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam.

Baada ya kuhoji hayo, Prof. Kabudi alijibu “hakuna mahakama yoyote inayoinyang’anya mahakama nyingine kesi sababu mahakama sio ambulance haifuati mgonjwa bali inapelekewa kesi, kwa hiyo kama kuna kesi inayohusu raia wa Tanzania Zanzibar katika Mahakama Kuu ya Tanzania, yupo aliyeipeleka.”

1 Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Rais Samia: Matumizi ya nishati safi sio anasa, ladha ipo

Spread the loveRAIS Samia Suluhu Hassan amesema matumizi ya nishati safi kwa...

Habari za SiasaTangulizi

Samia: Kuanzia Agosti marufuku kutumia mkaa, kuni

Spread the loveRAIS Samia Suluhu Hassan amemuagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya...

Habari za SiasaTangulizi

Mwendokasi Kigogo – Segerea kujengwa awamu ya 5

Spread the loveNaibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (TAMISEMI), Festo Dugange...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Rais Samia ni Mzanzibari: Shida Iko Wapi?

Spread the loveTAIFA linakabiliwa na upungufu wa fikra sahihi. Upungufu huu unaonekana...

error: Content is protected !!