MAMLAKA ya Wawasiliano Tanzania (TCRA), imesitisha kwa muda matumizi ya bei mpya ya vifurushi vya data, ili watoa huduma wapange upya bei hizo kwa ajili ya kulinda maslahi ya watumiaji. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Bei hizo zimeanza kutumika leo Ijumaa tarehe 2 Aprili 2021.
Bei hizo, zimezua mjadala mkali mtandaoni kutokana na vifurushi vya data kupungua tofauti na awali.
Ni matokeo ya matumizi ya kanuni ndogo za gharama na tozo za vifurushi, utangazaji wa huduma maalum, zilizoandaliwa na TCRA.
Taarifa iliyotolewa leo usiku Ijumaa na Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, James Kilaba imesema, “TCRA imesitisha kwa muda matumizi ya bei mpya ya vifurushi vya data ili kutoa nafasi kwa watoa huduma kupanga upya bei za vifurushi kwa ufanisi na kufanya uchambuzi wa kina kwa ajili ya kulinda maslahi ya watumiaji.”
Tarehe 2 Machi 2021, James Kilaba, Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, akizungumzia mabadiliko hayo, alisema zitaanza kutumika tarehe 2 Aprili 2021, ambayo ni leo.
Miongoni mwa yaliyomo katika kanuni hizo ni pamoja na huduma zote za vifurushi, lazima zipate vibali vya TCRA na vitadumu kwa siku 90, kabla ya kufanyika kwa mabadiliko mengine.
Hii ina maana kuwa, kwa bei za vifurushi vilivyoanza kutumia leo Ijumaa, vitadumu kwa siku 90, sawa na miezi mitatu kwa mujibu wa kanuni hizo.
Pia, kanuni hizo zinaelekeza, mtoa huduma atatakiwa kutoa taarifa pale matumizi ya kifurushi husika yatakapofika asilimia 75, na pale kifurushi kitakapokwisha.
Leave a comment