JOHN Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, anakuwa kiongozi wa tatu wa juu wa taifa hilo, kufariki dunia ndani ya kipindi cha mwezi mmoja. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa za kifo cha Rais Magufuli, zimetolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Mama Samia Suluhu Hassani akisema zimetokana na matatizo ya mfumo wa umeme kwenye moyo.
Alisema, Rais Magufuli (61), amefariki dunia, majira ya saa 12 jioni, jana Jumatano, tarehe 17 Machi, katika Hospitali ya Mzena, mkoani Dar es Salaam.
Mama Samia alitangaza siku 14 za maombolezo na bendera zitapepea nusu mlingoti huku taratibu za mazishi zikiendelea.
Wengine waliofariki dunia kabla ya Rais Magufuli, ni aliyekuwa Makamo wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad na aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi.
Maalim Seif (77) – mwamba wa kisiasa na vuguvugu la demokrasia barani Afrika – alihitimisha safari yake ulimwenguni, Jumatano ya tarehe 17 Februari 2021, saa 5:26 asubuhi, katika hospitali ya taifa Muhimbili, jijini Dar es Salaam.
Alizikwa siku iliyofuata, tarehe 18 Februari, kijijini kwake, Mtabwe, kisiwani Pemba.
Akitangaza kifo cha kiongozi huyo, ambaye alikuwa Makamo wa Kwanza wa Rais Visiwani, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi alisema, Maalim Seif, alikuwa amelazwa katika hospitali ya Muhimbili, tokea 9 Februari mwaka huu, kwa ajili ya matibabu.
Mbali ya kuwa Makamo wa Kwanza wa Rais Visiwani, Maalim Seif alikuwa mwenyekiti wa Chama cha ACT Wazalendo.
Kabla ya kufikishwa Muhimbili, Maalim Seif alikuwa amelazwa kwenye hospitali ya Mnazi Mmoja, Unguja.
Chama chake cha ACT- Wazalendo, kilieleza kuwa alipata maambukizi ya virusi vya Corona.
Naye Balozi Kijazi, alifariki dunia, saa 3/”:10 usiku wa tarehe 17 Februari, kwenye hospitali ya Benjamin Mkapa, mjini Dodoma, ambako alikuwa amelazwa kwa matibabu.
Mwili wa Balozi Kijazi, ulizikwa nyumbani kwao, Korogwe mkoani Tanga.
Mwingine aliyefariki dunia, ni aliyekuwa gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Prof. Benno Ndulu na aliyekuwa katibu mkuu wizara ya fedha, Dk. Servacius Likwelile.
Prof. Ndullu (71), alifariki dunia, Jumatatu tarehe 22 Februari katika hospitali ya Kairuki, mkoani Dar es Salaam.
Naye Dk. Likwelile, ambaye alikuwa mhadhiri wa idara ya uchumi Ndaki ya Sayansi ya Jamii, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), alifariki dunia, Februari 20 mwaka huu.
Taarifa za kifo cha Dk. Likwalile, zilitolewa na mkewe Vick Kamata, kupitia ukurasa wake wa kijamii wa Instagram akieleza mumewe ameugua kwa muda mfupi.
Tangu kufariki kwa viongozi hao, msimamo wa Serikli katika mapambano ya lugha ya virusi vya Corona nchini (COVID-19), ilianza kubadilika.
Hatua hiyo ilitoka a hasa baada ya viongozi wa madhehebu ya kidini, kutaka waamini wake, kuchukua tahadhari dhidi ya gonjwa hilo, ikiwemo kuvaa barakoa, kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima na kunawa mikono mara kwa mara na maji tiririka.
Hata hivyo, ukubwa wa orodha ya watu waliofariki dunia kutokana na changamoto ya upumuaji, ilisaidia kuisukuma serikali, kutangaza tahadhari kwa wananchi wake.
Akizungumza katika ibada ya kuuga mwili kitaifa wa Balozi Kijazi, kwenye viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli alitangaza siku tatu za maombi (Ijumaa, Jumamosi na Jumapili) kwa kufunga, kusali na kuomba ili Mungu atokomeze tatizo la ugonjwa wa kupumua.
Aliwaomba viongozi wa dini nchini, kuendelea kuwahamasisha waumini wao kufanya maombi hayo, “ili taifa lishinde kama lilivyoshinda katika maombi dhidi ya janga la mlipuko wa virusi vya corona mwaka jana.”
Alisema, “niwaombe viongozi wa dini kama mlivyokuwa mkifanya endeleeni kutangaza maombi tutashinda, tulishinda mwaka jana mpaka tukaingia uchumi wa kati na corona ipo.”
Leave a comment