MBUNGE wa Kibamba (CCM), Issa Mtemvu ameitaka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (Dawasa), kukamilisha kazi ya kufikisha maji kwa wananchi kwa kuwaunganisha na mitandao mikubwa ya maji ili kuharakisha upatikanaji wa huduma hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Mtemvu alitoa kauli hiyo jana Jumatano tarehe 6 Januari 2021, wakati wa ziara ya kutembelea miradi ya maji inayotekelezwa na Dawasa lengo likiwa ni kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi ipasavyo.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo iliyofanyika kwenye kata ya Kawe, Ubungo na Kibamba, Mtemvu alisema utekelezaji wa miradi ya maji kwa maeneo yote unaendelea vizuri.
“Hata hivyo, tumebaini uwepo wa changamoto mbalimbali zinazochelewesha upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi,” alisema
Mtemvu alisema, ziara imetokana na majadiliano yaliyotokana na kikao kazi cha Waziri wa Maji, Jumaa Aweso na wabunge 16 wa mikoa ya Dar es Salaam na Pwani wanaohudumiwa na Dawasa pamoja na menejimenti ya mamlaka hiyo.
Alisema bado kuna changamoto ya upatikanaji wa maji kwenye maeneo aliyotembelea, hususani kata ya Kibamba.
“Tumebaini kuna kazi ndogo iliyobaki ya kukamilisha maunganisho ya maji toka kwenye mtandao mkuu wa maji kwenda kwa wananchi na hivyo kuchelewesha upatikanaji wa maji kwa wananchi,” alisema.
“Tunatambua ipo nia njema kwa Dawasa kuanzia kwa mtendaji mkuu na mameneja wote ya kutatua changamoto za maji, tunaamini kazi iliyobaki ya kukamilisha maunganisho ya mabomba toka kwenye mtandao mkuu kwenda kwenye nyumba za wananchi itakamilika na wananchi watapata maji kikamilifu,” alisema.
Alisema ipo kazi kubwa inayofanyika ya utekelezaji wa miradi mikubwa inayoenda kumaliza changamoto ya maji kwa kata ya Kibamba, Ubungo na Kawe.
“Tunaimani kubwa na watendaji wa mamlaka kwamba wataenda kufanya kazi ya kutatua changamoto zilizoonekana kwenye maeneo yaliyopitiwa,” alisema mbunge.
Mtemvu alisema ziara imempa kujifunza namna Dawasa inavyoitahidi kushughulikia tatizo la upatikanaji wa maji kwenye sehemu korofi kwa kutumia njia ya mbadala na ya haraka.
Kwa upande wake, Meneja wa Mkoa wa Kihuduma Dawasa Ubungo, Gilbert Masawe alisema, wamejipanga kuhakikisha inafikisha huduma ya maji wa wananchi husika.
Alisema kwa sasa mpango uliopo ni ujenzi wa tanki kubwa la kuhifadhi maji eneo la mshikamano litakalo hudumia wakazi wa maeneo ya msakuzi yasiyokuwa na mtandao.
“Mamlaka inaendelea na zoezi la kufanya tathmini ya uwezo wa msukumo wa maji kwenye eneo la Mbezi Makabe kwa lengo la kufikisha maji kwa wakazi wote wa maeneo hayo,” alisema
Naye Meneja wa Mkoa wa Kihuduma Dawasa Kibamba, Elizabeth Sankere alisema, wanatekeleza mradi wa kulaza mabomba kwenye eneo la urefu wa kilomita 1.5 kwa lengo la kuwafikishia huduma ya maji wakazi wa hondogo mungu mwema.
Alisema mpaka sasa mkandarasi ameshaanza kazi ya kushughulikia mtandao wa mabomba ya maji na kazi inaendelea kwa ushirikiano na wananchi.
Kwa upande wake, Diwani wa Msigani, Hassani Mosha aliwataka wananchi wa kata ya Msigani kuwa na imani na Dawasa na wategemee mabadiliko makubwa kwa sababu mamlaka hiyo imeweka viongozi wapya kwenye maeneo yao wenye uwezo wa kutatua changamoto ya maji kwa ufanisi mkubwa.
“Nina imani kubwa kuwa Dawasa inayotekeleza miradi mikubwa ya maji, hawatashindwa kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji kwenye maeneo haya, na kwa kuwa ni mitaa mitaa michache yenye changamoto ya upatikanaji wa maji kwenye Kata hii,” alisema Mosha
Leave a comment