SAED Kubenea, Mgombea Ubunge kinondoni kupitia Chama cha ACT-Wazalendo ametaja masuala yanayokitesa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwenye kampeni za Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Kubenea ametaja sababu hizo jana Jumamosi tarehe 3 Oktoba 2020 katika mkutano wake wa kampeni Wilayani Kinondoni, Dar es Salaam.
Mwanasiasa huyo amesema, zuio la mikutano ya hadhara kwa takribani miaka mitano, kukandamizwa kwa wanasiasa wa upinzani, kuzuia mikutano ya bunge kurushwa mubashara, ndio kinachowapa shida CCM wakati huu.
“Ndio maana Rais John Magufuli na chama chake kinapata shida sana katika uchaguzi huu, walizuia mikutano ya hadhara miaka mitano, wakauzia bunge live, wakazuia wabunge wao wasiseme bungeni, wakakamata wapinzani na kuwafungulia kesi, wakanunua wabunge wa upinzani, wakifikiri shughuli imeisha kumbe ndio kwanza inaanza,” amesema Kubenea.
Kubenea amewaomba wananchi wa Kinondoni wamchague badala ya kuchagua Mgombea wa CCM, Abbas Tarimba akisema, wabunge wa upinzani wana uwezo wa kutimiza majukumu ya mbunge ambayo ni kuisimamia, kuishauri na kuiwajibisha Serikali inapokosea.
“Kazi za mbunge ni tatu, kusimamia Serikali, maana ya kusimamia mnajua ni lazima uwe na ushupavu na ujasiri wa kusimama na kumkemea mtu, mbili kushauri Serikali, tatu kuiwajibisha, hizo ndio kazi za mbunge ukiwa na mbunge unayetokana na CCM huwezi simamia Serikali hasa ya Magufuli, wabunge wa CCM wote wameufyata,” amesema Kubenea.
Kubenea ambaye kitaalamu ni mwandishi wa habari alisema, yeye yuko tayari kuwawakilisha vyema wananchi wa Kinondoni kwani uzoefu huo anao na matatizo ya jimbo hilo anayajua.
Amesema, Tarimba hawezi kwenda kuwawakilisha vyema kwani ataweka mbele maslahi yake na ya chama chake jambo ambalo litawafanya wana Kinondoni kutokuwa na msemaji na mwakilishi madhubuti ndani na nje ya Bunge.
Leave a comment