BERNARD Membe, Mgombea Urais wa Tanzania kupitia ACT-Wazalendo, amewataka wananchi wa Kilwa Mkoa wa Lindi, kuumuuliza maswali manne, mgombea urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Rais John Pombe Magufuli. Anaripoti Faki Sosi, Lindi … (endelea).
Mwanadiplomasia huyo, ameyatoa maswali hayo kwa wananchi wakati akihutubia mkutano wa kampeni za urais uliofanyika leo Jumatano tarehe 2 Septemba 2020 katika viwanja vya Bustani ya Mkapa, Kilwa Masoko.
Membe aliyepata kuwa waziri wa mambo ya nje wa Tanzania kati ya mwaka 2007 hadi 2015 enzi za utawala wa Rais mstaafu Jakaya Kikwete amesema, Rais Magufuli atakapofika Kilwa aulizwe maswali hayo.
Baadhi ya maswali hayo, Membe amesema, iko wapi mipango ya gesi kwa wananchi wa Kilwa, Lindi na Mtwara na akijibu swali hilo aulizwe jingine.
“Kwanini mikoa ya Kusini hakuna barabara ya kudumu, kwani hakuna barabara ya kutoka njia panda kwenda Pande kwa sababu alikuwa waziri wa Ujenzi na Miundombinu,” amesema Membe
Pia, Membe amesema swali jingine “tumuulize kwanini ameingilia soko la korosho, ufuta na mbaazi.”
Amesema, mawakala wa korosho maarufu kama kagomba atawaruhusu kufanya biashara endapo watamchagua katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020.
Kuhusu suala la uvuvi,Membe ameahidi kukuza maslahi ya uvuvi pamoja na kuzuia kuwachomea nyavu wavuvi.
“Mimi sitachoma moto nyavu zenu, mtavua samaki, hayupo atakayechoma moto nyavu kama ni Waziri nitamfukuza siku hiyo hiyo. Huku akiwauliza wananchi nilonge nisilonge nao wakimjibu..longa” amesema Membe
Awali, mgombea mwenza, Profesa Omar Fakih Hamad amesema, ili taifa listawi ni lazima kuimarisha muungano kupitia chama hicho.
Amesema, ili safari ya maendeleo ya Taifa ni lazima kuwepo kwa muungano wa haki.
Profesa Hamad amesema, ili Muungano uwe na haki kwa pande zote kati ule wa Tanzania Visiwani na Tanzania Bara ni lazima wakiondoe Chama Cha Mapinduzi (CCM) madarakani.
Amesema ujumbe huo ametoka nao Visiwani Zanzibar na kwamba kuiondoa CCM kutastawisha Muungano wenye haki.
Amewataka wapiga kura waichague ACT-Wazalendo kwa kuwa chama hicho kina nguvu na kwamba CCM imechoka.
“Punda akiwa mbovu hata ukibadirisha masogi mara kumi hataweza kuimarika . ACT-Wazalendo ni punda mzima,” amesema
Amesema Membe atakapoingia madarakani atahakikisha Muungano utakuwa wenye haki.
Leave a comment