BEI ya mafuta ya Petroli na Dizeli yaliyoingizwa nchini kupitia Bandari ya Dar es Salaam, imeongezwa kuanzia kesho Jumatano tarehe 1 Julai mwaka huu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa ya mabadiliko hayo imetolewa na Godfrey Chibukunje, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo tarehe 30 Juni 2020.
Wakati bei za rejareja ikiongezeka kwa Sh. 173 kwa lita sawa na asilimia 11.38, bei za jumla zimeongezeka kwa Sh. 172.39 kwa lita, sawa na ongezeko la asilimia 12.35.
Bei ya mafuta ya taa haijapanda, kwa kuwa hakuna mafuta ya taa yaliyoingizwa nchini kupitia bandari hiyo.
“Mabadiliko hayo yamechangiwa na mabadiliko ya bei ya mafuta katika soko la dunia,” imeeleza taarifa ya Ewura.
Kuhusu Mikoa ya Kaskazini (Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara) ambayo hutumia mafuta yanayopitia Bandari ya Tanga, bei za mafuta hazijapanda, kwa kuwa hakuna mafuta yaliyoingizwa nchini kupitia bandari hiyo.
Katika Mikoa ya Kusini, bei ya mafuta ya Petrol na Diesel imebaki palepale kwa kuwa, hakuna mafuta yaliyoingizwa nchini kupitia bandari hiyo.
Kutokana na upungufu wa mafuta katika Mikoa ya Kusini, wamiliki wa vituo vya mafuta katika Mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma wameshauriwa kununua mafuta hayo kutoka Dar es Salaam.
“Wamili wa vituo vya mafuta wanashauriwa kununua mafuta hayo kutoka Dar es Salaam, na hivyo bei za rejareja za Petroli kwa mikoa hiyo zinatokana na gharama za mafuta hayo kutoka Dar es Salaam. Pamoja na gharama za usafirishaji za mafuta hayo hadi mikoa husika,” inaeleza taarifa ya Ewura.
Leave a comment