Thursday , 2 May 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Jussa amwendesha Zitto 
Habari za Siasa

Jussa amwendesha Zitto 

Spread the love

ISMAIL Jussa, mgombea nafasi ya Uongozi Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, ametumia vyema mdahalo wa kuwapima wagombea wa chama hicho, kuonesha udhaifu wake, chini ya uongozi wa  Zitto Kabwe, anayetetea nafasi hiyo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam…(endelea).

Jussa ameutumia vyema mdahalo huo uliofanyika leo tarehe 13 Machi 2020 jijini Dar es Salaam, kueleza maeneo ambayo ACT-Wazalendo haikufanya vizuri.

Jussa alikosoa kitendo cha chama hicho kushikiliwa na nguvu ya mtu mmoja, huku akijinadi kwamba, akipewa ridhaa ya kuwa kiongozi wake, atahakikisha nguvu hiyo inasambaa kwa wanachama wengi.

Katika kuipa nguvu hoja yake hiyo, Jussa ametolea mfano kitendo cha ACT-Wazalendo kuwa na mbunge mmoja ambaye ni kiongozi, akisema kwamba si sahihi kwani akikosekana bungeni kutokana na kubanwa na majukumu ya ujenzi wa chama, kinakosa muwakilishi bungeni.

Jussa amesema kitendo cha ACT-Wazalendo kuwa na mbunge mmoja, ni ishara ya kwamba kiongozi aliyeko madarakani sasa, ameshindwa kutekeleza wajibu wake wa kueneza chama ili kipate ridhaa ya wananchi.

Amesema kama atachaguliwa kuwa kiongozi, atahakikisha chama hicho kinapata wawakilishi wengi bungeni.

“Sidhani kama kuwa na mbunge mmoja ni mafanikio kwangu, nguvu ya chama ingeonekana kuwa na wabunge wengi. Nakubali ingelikua jukumu la kiongozi kuwa msemaji ingeishia hapo. Mengi katika mambo naita ni mapungufu tunapaswa kuyarekebisha.

Mengi katika utendaji naamini kuna maeneo mengine sikuyaona kama ameyafanya. Naamini anafaa kukaa benchi Jussa niongoze,” amejinadi.

Jussa amesema ACT wazalendo kinahitaji kuenezwa Tanzania na nje ya nchi, na kwamba anafaa kupewa uongozi wa chama hicho, kwa kuwa ana uzoefu katika masuala hayo, .

“Nina uzoefu katika Mahusiano ya kimataifa na mikakati ya kisiasa. Hivyo nikichaguliwa nitakitumikia vizuri chama. ACT kuna baadhi ya maeneo hayajafanyiwa kazi. Ikiwemo kuendesha siasa katika maeneo yake ya asili. Lazima kisambae hakipaswi kuwa chama cha maeneo maalumu. Kazi hiyo naweza kuifanya mimi katika kuimarisha,” amejinasibu Jussa.

Akipangua hoja hizo, Zitto amesema kazi za utendaji wa chama si za kiongozi mkuu, nafasi anayoishikilia yeye, bali anayepaswa kulaumiwa kwa udhaifu wowote ni Katibu Mkuu, mwenye wajibu wa utendaji wa kazi za chama.

“Kazi ya utendaji wa chama si ya kiongozi ni ya katibu, hivyo wa kuondolewa ni katibu mkuu,” amejitetea Zitto.

Zitto amesema ACT-Wazalendo chini ya yongozi wake, imekuwa imara ndani ya muda mchache, sababu iliyomfanya Jussa na wenzake kutoka Chama cha Wananchi (CUF), wakikimbilie chama hicho.

Kiongozi huyo wa ACT-Wazalendo amesema, Jussa alikipenda chama hicho hadi kuungana nacho, kwa kuwa kina ushawishi katika kufanya mabadiliko ya siasa nchini.

“Na ni dhahiri siwezi kubisha kwamba leo tuna uwezo wa kusema hivyo, sababu ya kina Jussa kuwepo ACT, lakini pili walifanya utafiti wa vyama vingi wakaona chama ambacho kina muelekea kinaweza kufanya mabadiliko katika nchi ni ACT Wazalendo.

Na wakati wanafanya hivyo kiongozi ni mimi, na ndio maana nilimuuliza mwenzangu una nini, kwa nini unagombea. Mimi nimefanya chama kinakua we una nini?” amepangua hoja Zitto.

Zìtto amejitetea zaidi kwamba, alifanya kazi kubwa ya kukieneza chama hicho ndani na nje ya Tanzania, ndiyo maana Jussa alipata fursa ya kualikwa na vyama vya upinzani vya kimataifa, kushiriki mikutano ya siasa kupitia ACT-Wazalendo.

Amesema katika uongozi wake, ACT-Wazalendo ilifanikiwa kupata madiwani zaidi ya 42 na kushililia halmashauri moja.

Zitto amejinadi zaidi kuwa  “Mazingira ya sasa inabidi kupata kiongozi wa upinzani anayemkabili vilivyo kiongozi wa CCM. Nafasi hii sigombei kwa ajili ya ACT, ni kwa ajili ya Tanzania nzima.”

Kuhusu mapungufu aliyoyaraja Jussa, Zitto ameahidi kwamba, akipewa tena nafasi ya kuongoza atayarekebisha. Huku akisisitiza kuwa, alifanya kazi kubwa ya kukijenga ACT-Wazalendo, hivyo sasa atafanya kazi ya kukiimarisha

Chama cha ACT-Wazalendo kinatarajia kufanya uchaguzi Jumapili ya tarehe 15 Machi 2020.

 

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Spika Tulia aibana Serikali mafao ya wastaafu Jumuiya ya Afrika Mashariki

Spread the loveSPIKA wa Bunge, Dk. Tulia Ackson ameitaka Serikali kufanya tathimini...

Habari za Siasa

Serikali yawapa maagizo Ma-RC udhibiti magonjwa yasiyoambukiza

Spread the loveWAKUU wa mikoa nchini wametakiwa kuandaa utaratibu wa kuwawezesha wananchi...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Mavunde ataja malengo “Vision 2030”

Spread the loveWAZIRI wa Madini amesema dhana ya “Vision 2030” inakusudia kuiendeleza...

Habari za Siasa

Mavunde aomba bilioni 231.9 bajeti wizara ya madini

Spread the loveWAZIRI wa Madini, Anthony Mavunde leo Jumanne amewasilisha hotuba ya...

error: Content is protected !!