CHAMA cha ACT-Wazalendo kimesema kitaipeleka serikali mahakamani, iwapo itaendelea na msimamo wake wa kuzima laini za simu zisizosajiliwa kwa mfumo wa alama za vidole. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Ado Shaibu, Katibu wa Itikadi na Uenezi ACT-Wazalendo, ametoa kauli hiyo leo tarehe 20 Januari2020, wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Amesema, iwapo serikali itachukua hatua hiyo, itaathiri uchumi wa wananchi pamoja na pato la taifa.
Pia, itakuwa imeonea wananchi wasiokuwa na namba za kitambulisho cha taifa kinachotolewa na Mamlaka ya Vitambulisho nchini (NIDA), kwa ukosefu huo umetokana na utendaji wa mamlaka hiyo kusua sua.
“Uamuzi huu una hasara kwa uchumi, serikali kupata mapato. Tunadhani serikali ambayo imesababisha hili inaweza kurudi kwenye akili zake na kuacha uamuzi huo. Kama watatekeleza tutachukua hatua katika muda usiozidi wiki moja maana kuna utaratibu wa kisheria,” amesema Ado.
Ado amesema hadi sasa Watanzania zaidi ya milioni 20 hawajasajili laini zao kwa mfumo huo, kutokana na sababu mbalimbali, hasa ukosefu wa namba za NIDA.
“Hii ina maana kuwa laini za simu 22,478,727 sawa na asilimia 46.3 zilikuwa bado hazijasajiliwa kwa mfumo wa alama za vidole. Iwapo uamuzi huu utatekelezwa wanancho hao wote watakosa mawasiliano,” amesema Ado.
Amesema maeneo yatakayoathirika na hatua hiyo ni pamoja na Mkoa wa Kigoma ambapo asilimia 73 ya wananchi ya wananchi bado hawajasajiliwa.
Ado ameishauri serikali kuiongezea bajeti NIDA ili iongeze ufanisi wake katika kuzalisha namba za vitambulisho.
Leave a comment