RAIS John Magufuli leo tarehe 24 Aprili 2019, anatarajia kuanza ziara ya kikazi ya siku mbili nchini Malawi. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa inaeleza kwamba, Rais Magufuli akiambatana na mkewe Mama Janeth Magufuli, wameondoka nchini kuelekea Malawi kwa ajili ya ziara hiyo ya kiserikali.
Taarifa hiyo inaeleza kwamba, Rais Magufuli anafanya ziara hiyo kufuatia mwaliko aliopewa na Rais wa Malawi, Profesa Arthur Mutharika.
“Rais amagufuli akiwa na Mkewe Mama Janeth Magufuli ameondoka katika Uwanja wa Ndege wa Kikataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam na atapokelewa rasmi na mwenyeji wake Rais Mutharika,” inaeleza sehemu ya taarifa ya Musigwa.
Katika ziara hiyo, Rais Magufuli anatarajia kutembelea maeneo mbalimbali ya kihistoria nchini Malawi, pamoja na kufungua msimu wa soko la tumbaku na kuzungumza na wadau wa zao hilo.
“Atafanya mazungumzo na mwenyeji wake Rais Mutharika na jioni atahudhuria dhifa ya kitaifa aliyoandaliwa kwa heshima yake na Rais Mutharika,” inaeleza taarifa ya Msigwa.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa, baada ya ziara hiyo kumalizika kesho tarehe 25 Aprili 2019, Rais Magufuli atafanya ziara ya kikazi ya siku nane mkoani Mbeya.
Leave a comment