MFANYABIASHARA na mmiliki wa mabasi ya Batco jijini Mwanza Baya Kusanja Malagi pamoja na benki ya CRDB wanadaiwa kula njama kwa pamoja na kutapeli hoteli ya Tai Five iliopo kona ya Bwiru mkoani Mwanza. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Hoteli ya Tai Five inamilikiwa na mfanyabiashara Wilson Christopher Tarimo.
Taarifa za kuaminika zinasema kuwa benki ya CRDB ilifanya kosa la kumkopesha hoteli hiyo mfanyabiashara huyo kwa kiasi cha Sh. 1 bilioni tarehe 28 Juni, 2017.
Nyaraka zilizopatikana zinaonyesha kuwa CRDB walichukua hati za Wilson Tarimo CT namba 3001 za Tai Five Hoteli LTD na CT namba 2898 za Wilson Christopher Tarimo ambazo walimpa Kusanja Malagi kukopea benki jambo ambalo linaonesha utapeli katika benki hiyo.
Akizungumza na Mtandao huu, mmiliki wa hoteli hiyo, bwana Wilson Tarimo alisema CRDB walichukua hati zake na kumpa mfanyabiashara huyo kwa njia za udanganyifu.
Amesema kuwa utapeli uliofanywa na CRDB pamoja na Kusanja ni utapeli ambao haujawahi kutokea duniani kote kwani kutoa hati za mtu na kumpa mwingine kukopea fedha ni wizi ambao hauwezi kufumbiwa macho.
Tarimo amesema hoteli yake aliijengwa kwa gharama ya Sh. 5.5 bilioni tangu mwaka 1993 hadi 2008 lakini anasikitika kuona CRDB wanamkopesha Kusanja Malagi kwa bilioni moja.
Pia Tarimo amesema kuwa CRDB walishirikiana na mfanyabiashara huyo kutapeli hoteli yake kwa kughushi nyaraka za hati zake ambazo zimetajwa hapo juu.
“Hati za Tai Five zimechukuliwa na CRDB wakampa Baya Kusanja kukopea kwao fedha ili amiliki hoteli yangu, yaani kwa sasa mabenki yanatapeli watu nyumba zao badala ya kuwasaidia,” alisema Tarimo.
Amesema sasa ameamua kukimbilia mahakamani ili kwenda kupata haki yake kwani ameona bila uficho benki hiyo imemtapeli hoteli yake.
Tarimo amesema anaamini kuwa haki yake itatendeka kwa sababu mwalimu wake wa Sengerema Sekondari, Rais mpendwa John Magufuli ni mpenda haki na msimamia ukweli.
MwanaHALISI Online ilimtafuta Baya Kusanja Malagi kwa njia ya simu kwa siku mbili mfululizo ili kuzungumzia suala hilo, alipopokea simu na kuulizwa juu ya madai hayo alikata simu na kila alipopigiwa tena hakupokea.
Leave a comment