MBUNGE wa Iringa Mjini Peter Msigwa ameshangazwa na kibwagizo kilichokuwa kikitumiwa na vijana wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) cha kusema upinzani unakufa, kwenye mkutano wa tisa wa UVCCM Taifa uliofanyika siku mbili katika ukumbi wa Chuo Cha Mipango, Dodoma, anaandika Shabani Matutu.
Katika mkutano huo ambao uliwachagua viongozi wao wapya akiwemo, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana UVCCM, Kheri James walikuwa wakitumia kibwagizo kinachosema kwamba ‘upinzani unakufa’ jambo lililomkera Msigwa.
Msigwa alisema “Fine! tukubaliane Kuwa upinzani unakufa! Jambo la kujiuliza hivi upinzani ukifa upinzani zitaongezeka ajira ngapi! Umaskini utapungua kwa kiwango gani? Haki za binadamu zitalindwa kwa kiwango gani?
Anaongeza kuwa, “tujiulize utawala bora utaimarika kwa kiwango gani? Demokrasia itaimarishwa kwa kiwango gani? Uhuru wa kutoa mawazo na vyombo vya habari utaimarika kwa kiwango gani! Wanatakiwa watambue kuwa haya yote hayana chama.”
Mbunge huyo alisema kwamba mategemeo yake alitarajia CCM wangeutumia mkutano huo kwa kuleta majibu ya masuala hayo muhimu ambayo kila mwananchi angependa kuona majibu yake kwa vitendo.
Wengine waliochaguliwa katika uchaguzi huo ni Tabia Mwita aliyechaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa UVCCM na viongozi wengine waliotangazwa katika mkutano huo ni wajumbe wa Halmashauri Kuu na Mkutano Mkuu wa UVCCM.
Leave a comment