MKUTANO ulioitishwa leo na Jukwaa la Wahariri (TEF) na Waandishi wa Habari umegeuka kuwa kituko baada ya upande mmoja uliotarajiwa kuomba radhi kukataa kufanya hivyo, anaandika Hamisi Mguta.
Katika mkutano huo ulioitishwa na TEF na mwentekiti wake, Theophil Makunga jijini Dar es Salaam, umemalizika huku ukiacha maswali mengi kwa waandishi wa habari bila majibu.
Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Machi 3 mwaka huu, akiwa ameongozana na askari wenye silaha anadaiwa kuvamia ofisi za Televisheni ya Clouds kwa lengo la kutisha waandishia kwa maslahi binafsi.
Leo TEF imetangaza kumsamehe Makonda, baada ya kumsusia kuandika habari zake tangu alipovamia ofisi za Clouds, huku yeye mwenyewe akikataa kuomba radhi kutokana na kosa analodaiwa kulifanya.
Theophil Makunga, Mwenyekiti wa Jukwawa hilo amesema waliamua kuzuia waandishi wasiandike habari za Makonda kwa madai ya kuona umuhimu wa usalama wa nchi ili wengine wasiweze kupata nafasi ya kiufanya kitendo kama kile, lakini baada ya mazungumzo wameona wamsamehe.
“Tukasema ngoja tuangalie kinachofuata nini? baada ya mazungumzo tukakubaliana kweli hiyo hali siyo nzuri kwa hiyo isirudiwe tena mbele ya safari,” amesema Makunga.
Hata hivyo, Makonda alionyesha kituko mbele ya waandishi wa habari, baada ya kukataa kuomba msamaha akisema haoni kosa alilolifanya.
“Sitaomba radhi, narudia tena kwa herufi kubwa, hukumu imetoka kwa upande mmoja na hawakutoa nafasi ya kusikiliza upande wa pili kwa hiyo waliachia fursa ya upande wa pili kuomba au kupata taarifa za kutosha ili kujua dira kamili.
“Askari nilionao wana kazi mbili, kuchunguza mwenendo wangu kama nafanya kazi kwa taratibu na kanuni na pili ni kulinda usalama na hata hapa tulipo wapo,” amesema Makonda.
Kwa upande wa Mkurugenzi wa vipindi wa Clouds TV, Ruge amesema anawalaumu TEF kwa kumuita katika mkutano huo wakati suala linaloamuliwa linahusu TEF na Makonda.
Leave a comment