JUJU Danda, Katibu Mkuu wa Chama cha NCCR – Mageuzi amesema hali ya demokrasia nchini Tanzania kwa sasa siyo nzuri kutokana na Serikali ya awamu ya tano kuvitumia vyombo vya dola kukandamiza demokrasia, anaandika Pendo Omary.
Danda ameimbia MwanaHALISI Online, “marufuku ya mikutano ya hadhara kwa vyama vya siasa iliyotolewa tarehe 7 Mei, 2016 ni kinyume cha Ibara ya 20 (1) ya Katiba ya Tanzania.
“Ibara hiyo inasema kila mtu anao uhuru wa kukutana na watu wengine kwa hiari yake na kwa amani, kushirikiana na watu wengine, na kwa ajili hiyo kutoa mawazo yake hadharani na kuanzisha na kujiunga na vyama au mashirika yaliyoanzishwa kwa madhumuni ya kuhifadhi au kuendeleza imani au maslahi yake au maslahi mengineyo,” amenukuu.
“Jeshi la Polisi limeruhusu mikutano ya ndani ambayo ni gharama kubwa sana kuiandaa na kuiendesha. Vinavyoumia ni vyama vichanga visivyo na raslimali za kutosha, lakini licha ya yote hayo haimanishi vyama vyetu vitakufa.
Danda amezungumzia hatua ya Ofisi ya Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI) hivi karibuni kumuita Edward Lowassa, Waziri Mkuu Mstaafu kwa ajili ya mahojiano kuhusu kile kilichodaiwa kuwa ni uchochezi.
Lowassa ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), alihojiwa kwa tuhuma za uchochezi baada ya kutoa kauli ya kumtaka Rais John Magufuli kutafakari upya hatma ya Mashekh wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislam Zanzibar maarufu kama Uamusho.
“Jeshi la Polisi lisitumike. Nimesikitishwa sana na hatua ya polisi kumuita Lowassa kumhoji kwa masuala ya kawaida. Ikumbukwe kuwa yeye ni waziri mkuu mstaafu pia ni Rais wa wakati wowote ujao. Huku ni kungilia uhuru wa mtu kutoa maoni yake,” ameeleza Danda.
Amepongeza hatua ya serikali kujitathimini kuhusu mikataba ya kifisadi hata hivyo, amesema changamoto ya ufisadi inatokana na ubovu wa Katiba.
“Mtu mmoja hawezi kutegemewa kuchukua hatua. Ni lazima watu waogope Katiba na sheria kuliko kumuogopa rais. Kama Rais anataka watu wamuunge mkono ni lazima afufue mchakato wa Katiba mpya.
“Tumekuwa na mfumo wa uchumi unaotumikia siasa. Tunao watawala ambao ni zao la siasa. Ndiyo wanaingia kwenye maamuzi na wanasiasa hawataki kuziamini taasisi za kiserikali zinazoongozwa na wataalamu. Hii pia ni sehemu ya changamoto,” amesisitiza Danda.
Leave a comment