KITENDO cha viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kumtambulisha Isihaka Juma Karanda kuwa ni mwenyekiti wa chama cha ACT Wazalendo, ilikuwa ni kumdanganya Rais John Magufuli mbele ya hadhara, anaandika Yasinta Francis.
Isiahaka alitangazwa kuihama ACT na kujiunga na CCM juzi, katika jukwaa ambalo Rais Magufuli alikuwa akihutubia wananchi. Aliyempokea ni Humphrey Polepole, Katibu wa NEC- Itikadi, na Uenezi Taifa, hata hivyo, chama cha ACT Wazalendo kimesema Rais alidanganywa na viongozi wa CCM.
Mrisho Swagara, mwenyekiti halisi wa ACT Wazalendo Mkoa wa Pwani, amesema kitendo kilichofanywa na viongozi wa CCM mkoa wa Pwani kwa kushirikiana na Polepole ni cha aibu, na ni hadaa na propaganda iliyomdhalilisha Rais Magufuli.
“Kumtangaza mtu aliyedai ni mwenyekiti wa ACT Wazalendo mkoa wa Pwani ni cha uongo wa dhahiri, na ni propaganda za kitoto za Polepole.
“Mtu waliyemtambulisha si mwenyekiti wa ACT na hana nafasi yoyote katika kamati ya uongozi ya mkoa wa Pwani na si mwanachama kabisa wa chama hicho. Mimi ndiyo mwenyekiti wa ACT Wazalendo Mkoa wa Pwani,” amesema Swagara.
Amekitaka Chama Cha Mapinduzi na viongozi wake, kubuni njia za kutatua matatizo yanayowakabili watanzania kama uhaba wa dawa hospitalini, hali ngumu ya maisha, kukosekana ajira badala ya kutengeneza propaganda za uongo na upotoshaji.
“Ni muhimu watanzania tutumie muda huu kuhoji juu ya masuala muhimu kama huduma za afya, ajira kwa vijana na mfumuko mkubwa wa bei,” amesema Swagara.
Leave a comment