WATU 18 abiria waliokuwa safarini kutoka Dar es Salaam kwenda Arusha kwa kutumia gari aina ya Coaster, wamenusurika kifo baada dereva wa gari hiyo kupoteza mwelekeo na kusababisha gari hiyo kupinduka na kutumbukia korongoni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro … (endelea).
Ajali hiyo iliyotokea leo mchana katika eneo la Hedaru wilayani Same mkani Kilimanjaro, imesababisha majeruhi 18 huku sita kati yao wakihamishiwa katika hospitali ya Rufaa KCMC baada ya kuwa katika hali mbaya.
Daktari wa zamu katika hospitali ya wilaya ya Same, Alfred Seti amesema majeruhi wengine 10 wanaendelea kupatiwa matibabu katika hospitali hiyo huku wawili wakitibiwa katika kituo cha afya Hedaru.
Mkuu wa Wilaya ya Same, Kasilda Mgeni ambaye amefika kuwajulia hali majeruhi hao, amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kuongeza kuwa chanzo ni uzembe wa dereva ambaye hajulikani alipo kwani baada ya ajali kutokea alitoroka na kutokomea kusikojulikana.
Amesema ajali hiyo imehusisha gari aina ya Toyota Coster yenye namba za usajili T819 DVD huku chanzo kikielezwa kuwa ni uzembe wa dereva kutozingatia sheria na alama za barabarani.
Aidha, amewataka madereva kuongeza umakini hasa wanapofika eneo la wilaya hiyo huku akitoa wito kwa abiria nao kuwa na tahadhari kutoa taarifa kufichua madereva wanaokiuka sheria, kuepusha madhara kama hayo.
Wakizungumza kwa shida baadhi ya majeruhi hao wamesema chanzo ni uzembe wa dereva kutokuwa makini kwani hata kabla ya ajali alikuwa hafuati taratibu za alama za barabarani.
Leave a comment