Thursday , 2 May 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Kambi Maalim Seif: Tutampa chama Lipumba
Habari za SiasaTangulizi

Kambi Maalim Seif: Tutampa chama Lipumba

Spread the love

KAMBI mbili ndani ya Chama cha Wananchi (CUF) zinaendea kuminyana huku kila moja ikishindwa kujua tamati ya mgogoro ndani ya chama hicho. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).

Kambi ya Maalim Seif Sharif Hamad na ile ya Profesa Ibrahimu Lipumba, mwenyekiti wa chama hicho taifa anayetambuliwa na Msajili wa Vyama vya Siasa zinakokotana mahakamani.

Mbarara Maharagande, Naibu Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano ya Umma ya chama hicho kutoka kambi ya Maalim Seif amesema, mahakama itaamua.

“Mahakama itaamua hatma ya mgogoro wetu,” Maharagande amemweleza mwandishi wa habari hii na kwamba, uamuzi wa mahakama ndio unaosubiriwa.

Mwandishi alitaka kujua hatma ya mgogoro huo ambao umedumu kwa muda mrefu sasa. Maharagande anasema, yeye na wale wanaomuunga mkono Maalim Seif watakuwa radhi kumwachia chama Prof. Lipumba iwapo mahakama itaona kuwa, ndio mwenye haki.

“Mahakama ikiamua kuwa haki ni upande wa Lipumba tutawaachia chama,” amesema Maharagande na kuongeza “lakini sisi tunaimini na mahakama, itatupa haki yetu.”

Kupasuka kwa CUF kumesababisha pia kupasuka kwa viongozi wa juu wa chama hicho ambapo Naibu Katibu Mkuu wa sasa, Magdalena Sakaya amebaki kwa Prof. Lipumba huku Naibu Katibu Mkuu aliyepita, Julisu Mtatito akimuunga mkono Maalim Seif.

Maharagande anasema, kesi zipo kwenye hatua ya usikilizwaji wa mashahidi, mahakama ikimaliza itatoa uamuzi kutokana ushahidi utakaotolewa.

Abdul Kambaya, Mkurugenzi wa Habari na  Mawasilino ya Umma CUF kwa upande wa Prof. Lipumba anajipa matumaini kwamba, mgogoro unakwenda kufikia tamati.

“Mgogoro huu unakwenda kufikia tamati, naamini hivyo,” amesema Kambaya ambaye ni miongoni mwa maofisa wa chama hicho aliye karibu zaidi na Prof. Lipumba.

Amesema kwamba, kutokuwepo kwa Katibu Mkuu anayewaunga mkono hakudhoofishi chama kwa kuwa, katiba ya chama hicho inampa nafasi ya usaidizi wa ngazi hiyo Naibu Katibu Mkuu.

“Yupo Sakaya, Naibu Katibu Mkuu hivyo chama hakiwezi kuwa dhoofu kwa sababu ya kutokuwepo Katibu Mkuu anayetuunga mkono.

“Katiba ipo wazi kuwa Katibu Mkuu anapokwepa majukumu yale basi yatahodhiwa na Naibu Katibu Mkuu, hivyo chama kitaendelea na shughuli zake,”amesema Kambaya.

Kambaya amesema, mgogoro uliopo CUF simpya na kwamba, vyama vingine ikiwemo CCM vimekumbwa na migogoro na hatimaye vilikaa sawa.

“Sio CUF pekee iliyokumbwa na mgogoro.vyama vya siasa ni kawaida kupitia migogoro mikubwa kama hii. Hata CCM ya sasa ndani kunafukuta lakini kwa kuwa ni chama tawala migogoro yake haiwezi kutoka nje na kufahamika na kila mtu.”

Mgogoro ndani ya chama hicho uliibuka Juni 13 mwaka 2016 mara baada ya Prof. Lipumba kutangaza kutengua barua yake ya kujiuzulu.

Prof. Lipumba alijuuzulu nafasi ya uenyekiti wa CUF mwaka 2015 wakati wa kuelekea uchaguzi mkuu kwa madai kuwa hakuridhishwa na uamuzi wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kumpa nafasi ya kugombea urais Edward Lowassa, aliyetoka CCM.

Ukawa unaoundwa na CUF yenyewe, Chadema), NCCR-Mageuzi, na NRD.

Mgogoro ndani ya chama hicho umekuwa ukiongezeka kila kukicha ambapo Julai 26 mwaka 2017  wabunge wanane wa  viti  maalamu kambi ya Maalim Seif waliondolewa bungeni baadaya Prof. Lipumba kuwavua uanachama. Wabunge hao wamekwenda mahakamani kupinga uamuzi huo.

Zipo kesi zaidi ya 10 zinazohusu migogoro ndani ya chama hicho  pamoja na kesi namba 23 ya mwaka 2017 kuhusu uhalali Prof. Lipumba kuwa mwenyekiti wa chama hicho, shauri namba 557 (lilifunguliwa na Shawaji Mketo-Mjumbe wa Kamati ya Uongozi CUF).

Nyingine ni kesi namba 558 iliyofunguliwa na Juma Mkumbi -Mjumbe wa Kamati ya Uongozi la CUF) mwaka 2017 ambapo chama hicho kinapinga uhalali wa  wajumbe wa bodi ya wadhamini iliyoundwa na Prof. Lipumba, kesi hii namba 13 ya mwaka 2017 iliyofunguliwa na Mbunge wa Malindi, Ali Salehe.

 Ipo kesi namba 20, 68 na 80 ya mwaka 2017 dhidi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya kuiomba mahakama  kuzuia ruzuku na fedha za chama hicho kutumiwa na Prof. Lipumba na kambi yake.

Kesi nyengine ni namba 21 ya mwaka 2017 ya wabunge 19 wanaopinga uenyekiti wa Prof. Lipumba. Lipo shauri namba 13 la mwaka 2017 liliyofunguliwa na Jorani Bashange-Mjumbe wa Kamati ya Uongozi CUF linalopinga bodi mpya ya wadhamini wa chama iliyoundwa na Prof. Lipumba.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Mavunde ataja malengo “Vision 2030”

Spread the loveWAZIRI wa Madini amesema dhana ya “Vision 2030” inakusudia kuiendeleza...

Habari za Siasa

Mavunde aomba bilioni 231.9 bajeti wizara ya madini

Spread the loveWAZIRI wa Madini, Anthony Mavunde leo Jumanne amewasilisha hotuba ya...

Habari za SiasaTangulizi

Lissu amjibu Fatma Karume kuhusu Rais Samia

Spread the love  MAKAMU Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema)...

Habari za SiasaTangulizi

Dk. Slaa: Watanzania iungeni mkono Chadema uchaguzi 2025

Spread the loveMWANASIASA mkongwe nchini Tanzania, Dk. Wilbroad Slaa, amewataka watanzania wakiunge...

error: Content is protected !!