MAUZO ya mazao aina ya choroko, Soya, Ufuta, Mbaazi sasa yatauzwa kwa mfumo wa stakabadhi ghalani kama ilivyo zao la korosho. Anaripoti Brightness Boaz, Dar es Salaam … (endelea).
Muongozo mpya wa mfumo wa biashara ya mazao hayo, umetolewa na Dk. Benson Ndiegea, Mkurugenzi wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika nchini (TCDC tarehe 24 Januari 2021, umeeleza namna mazao hayo yatakavyokusanywa kwenye magala, yatakavyouzwa na namna mkulima atakavyoweza kunufaika.
Amesema, TCDC kwa kushirikiana na Body ya Usimamizi wa Stakabali za Ghalani (WRRB) na Soko la Bidhaa Tanzania TMX, wameandaa muongozo wa biashara kwa kutumia mfumo wa stakabali za ghala kwa mwaka 2021.
“Mazao hayo yatakusanywa kwenye maghala ya vyama vya ushirika na kusafirishwa kwenda kwenye ghala kuu, mnada utafanyika ambapo taarifa za mazao yaliyopokelewa kwenye ghala kuu, itatumwa soko la bidhaa na kuuzwa kwa mnada kwanjia ya kimtandao (electronic),” amesema.
Kiongozi huyo amesema, mazao hayo hayalimwi kwa wakati mmoja hivyo, amewataka viongozi wote katika ngazi za mikoa, wilaya ambapo mazao hayo yanalimwa, kusimamia utekelezwaji wa mwongozo huo.
Dkt. Benson ameelezea namna malipo ya fedha yatakavyofanyika kati ya mkulima na wadau wengine baada ya mnunuzi kulipa.
“Mwongozo huu unaelekeza kwamba, malipo ya fedha yatafanyika ndani ya siku tano za kazi kwa wakulima na wadau wengine, baada ya mnunuzi kulipa malipo hayo kwenye akaunti ya soko la bidhaa na fedha zitahamishwa kwenda akaunti ya vyama vikuu vya ushirika ndani ya saa 12.
“Mwongozo unaelekeza kuwa, kila mkulima na wadau wengine watalipa fedha zao zote kupitia akaunti za benki ili kurahisisha malipo hayo kufanyika kwa wakati, hivyo kila mkulima anatakiwa kuwa na akaunti yake,” amesema.
Kiongozi huyo amesisitiza, kila mnunuzi ambaye anahitaji kununua mazao hayo, atatakiwa kwenda kujisajili kwenye soko la bidhaa Tanzania mtandaoni kupitia tovuti ili aweze kushiriki kwenye minada itakayokua inafanyika kila wiki.
“Mfumo huo unampa mkulima uhakika wa kuhifadhi kwa sababu, mazao hayo ukibaki nayo nyumbani, unaweza kuharibu thamani kutokana na njia ya uhifadhi,” amesema.
Leave a comment