TIMU ya Yanga imelazimishwa sare ya bao 1-1 dhidi ya JKT Tanzania katika mchezo wa mzunguko wa pili Ligi Kuu Tanzania Bara uliofanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri, Dodoma. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Mchezo huo ulishuhudiwa na viongozi mbalimbali wa Serikali akiwemo Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Harrison Mwakyembe na Katibu wa wizara hiyo, Dk. Hassan Abbas na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Mkuchika.
JKT ndio walikuwa wa kwanza kupata bao katika dakika ya 36 ya mchezo,kupitia kwa mlinzi wake wa kulia, Michael Aidan na Yanga kusawazisha katika kipindi cha pili kupitia kwa winga wao Patrick Sibomana dakika ya 76.
Mchezo huo ulikuwa wa nguvu na kugubikwa na vurugu nyingi kiasi cha beki wa kati wa Yanga, Lamine Moro kutolewa nje baada kuoneshwa kadi nyekundu kwa kumpiga teke kiungo wa JKT Tanzania, Mwinyi Kazimoto dakika ya 89.
Katika taflani hiyo Kazimoto nae aliotolewa nje kwa kadi nyekundu mara baada ya kuleta vurugu uwanjani hapo.
Lamine atakosa mchezo ujao dhidi ya Azam FC utakaopigwa siku ya Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Matokeo hayo yanaifanya Yanga kufikisha pointi 55 baaada ya kucheza michezo 29 na kusalia kwenye nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi hiyo.
Leave a comment