WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa anatarajiwa kufanya ziara ya kikazi ya siku tatu mkoani Songwe kwa lengo la kukagua miradi ya maendeleo, kuzungumza na wananchi pamoja na watumishi wa umma. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe…(endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 21 Novemba 2023, Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Dk. Francis Michael amesema kuwa, Waziri Mkuu atawasili mkoani Songwe kesho tarehe 22 Novemba 2023 na atahitimisha ziara yake tarehe 25 Novemba 2023 ambapo atetembelea Wilaya mbili za Ileje na Mbozi.
Dk. Francis alibainisha tarehe 23 Novemba 2023 Waziri Mkuu atakagua miradi miwili, kuweka mawe ya msingi ya miradi miwili pamoja na kuzungumza na wananchi wilayani Ileje.
Dk. Francis aliongeza kuwa tarehe 24 Novemba 2023, Waziri Mkuu atakuwa wilayani Mbozi ambapo atazindua mradi mmoja, kukagua miradi miwili, kuweka jiwe la msingi mradi mmoja pamoja na kuzungumza na wananchi.
Alibainisha kuwa siku ya tarehe 25 Novemba 2023 Waziri Mkuu atafanya majumuisho ya ziara yake, ikiwa ni pamoja na kuzungumza na watumishi wote wa Mkoa wa Songwe ambapo majumuisho hayo yatafanyika katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa.
Dk. Francis ameeleza kuwa ziara hiyo ya Waziri Mkuu mkoani humo ni muendelezo wa ziara aliyoifanya tarehe 13 hadi 16 Aprili, 2023 ambapo alitembelea Halmashauri tatu za Momba, Songwe na Tunduma na sasa anakuja kumalizia halmashauri ya Ileje na Mbozi.
Leave a comment