SERIKALI imesema watuhumiwa wa kesi 147 za rushwa wameachiwa huru baada ya kutopatikana na hatia katika kipindi cha mwaka mmoja. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yameelezwa leo Alhamisi tarehe 21 Aprili, 2022 bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Jenista Mhagama.
Amesema kesi hizo ni kati ya kesi 865 za tuhuma dhidi ya rushwa na ufisadi zilizoendeshwa mahakamani zikiwemo kesi mpya 305.
Amesema, kesi 338 ziliamuliwa mahakamani ambapo kesi 191 watuhumiwa walipatikana na hatia na kuhukumiwa kifungo au kulipa faini.
“Kesi 147 watuhumiwa wake hawakupatikana na hatia na kuachiwa huru. Kesi 527 bado zinaendelea mahakamani,” amesema Mhagama.
Katika hatua nyingine amesema Sh. bilioni 1.42 zimeokolewa kutokana na operesheni mbalimbali za uchunguzi uliofanyika kote nchini.
Amesema taasisi hiyo kwa kushirikiana na mamlaka nyingine imewezesha kutaifisha na kurejesha Serikalini fedha na mali zenye thamani ya Sh. bilioni 6.3 na dola za kimarekani 1,468,364 ambazo zinahusisha fedha, nyumba tano, viwanja sita na magari saba.
Leave a comment