Baadhi ya Walimu wa shule za msingi na sekondari katika Halmashauri ya Wilaya ya Ileje mkoani Songwe ‘wamemvamia’ Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo wakishinikiza kukubaliwa maombi yao ya kutaka kujitoa uanachama wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT). Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Walimu hao wamedai kuwa walituma maombi hayo ya kujitoa uanachama CWT miezi mitano iliyopita bila kupewa majibu sahihi.
Akizungumza na MwanaHALISI online kwa niaba ya walimu wenzake, Yodan Kalonge amesema amesema wamechukua hatua hiyo ya kwenda kwa mwajiri ‘Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri’ baada kuzungushwa na CWT kwa muda mrefu.
“Tulileta fomu za kujiondoa CWT na kuomba kujiunga na Chama cha Kutetea na Kulinda Maslahi ya Walimu Tanzania (CHAKUWAHATA) tangu Julai 2023 lakini shida CWT walileta pingamizi tusijiondoe, kwa hiyo mgogoro ndio ulipoanzia… tulikaa meza moja kufanya maridhiano lakini CWT bado hawataki,” amesema.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Herman Njeje amekiri kuwapokea walimu hao na kuwaelekeza kufuata taratibu.
Aidha, Mwenyekiti wa CHAKUWAHATA – Ileje, Kalonge Bwenda amesema chama kilichoanzishwa mwaka 2015, awali hakikusikika sana kwa kuwa walikuwa wanajipanga lakini sasa kasi ya kuboresha chama imeendelea kukua kutokana na migogoro inayoitafuna CWT.
“CHAKUWAHATA – Ileje tuliunda uongozi na kufanya mchakato wa usajili kisha kuutambulisha kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ambapo Julai 2023 alisema tuendelee kuwasilisha fomu za wanachama wanaojiunga.
“Mchakato ulifanyika kwa kufuata taratibu zote lakini ili tuendelee tukatakiwa kuwasilisha nakala za kujitoa uanachama wa CWT, wenzetu hao wakagoma kupokea nyaraka zetu, hata tulivyojaribu kutuma kwa EMS napo wakagoma kupokea,” amesema.
Amesema jumla ya walimu 172 kutoka CWT wanashinikiza kujitoa kwa sababu waliingizwa kwenye chama hicho bila hiyari yao wala kujaza fomu.
“Pili CWT wanatukata 2.5% kila mwezi katika mshahara wakati CHAKUWAHATA wanakata Sh 5,000 kwa kila mtu, hivyo nasi tunahitaji kuongeza kipato kwenye mishahara yetu.
“Tatu hatujui kuhusu mapato na matumizi ya CWT, mambo mengi yanaenda kienyeji na pia viongozi wa juu walimdharau Rais, wanateuliwa wanakataa, kuna nini hasa ambacho wanakipata ndani ya chama mpaka wanagomea uteuzi wa Rais?,” alihoji Mwalimu Yodan Kalonge.
Kwanini kujiunga na chama iwe lazima? Kwanini isiwe hiyari ya mfanyakazi? Sheria/katiba inasemaje?