SERIKALI imetoa mkono wa pole kwa familia 19 za wafiwa wa ajali ya ndege ya Precision Air iliyotokea jana tarehe 6 Novemba, 2022 na kusababisha vifo 19 akiwamo rubani na msaidizi wake. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Pia imeahidi kulipia gharama zote za mazishi za watu hao wanaotarajiwa kuzikwa maeneo mbalimbali nchini kulingana na maamuzi ya familia zao.
Hayo yamebainishwa leo na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa katika ibada maalum ya kitaifa ya kuaga miili ya watu hao 19 iliyofanyika katika uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera ambapo pamoja na mambo mengine ameagiza wakuu wa mikoa kusimamia mazishi hayo katika mikoa husika.
Awali akizungumza katika ibada hiyo ya kuoa heshima za mwishi, Mkuu wa mkoa huo wa Kagera, Albert Chalamila amesema uongozi wa Kiwanda cha Sukari Kagera umeunga mkono Serikali kwa kutoa mkono wa pole wa Sh milioni moja kwa familia hizo 19 za wafiwa.
“Kagera Sugar walisema tunakuunga mkono kila mwili ulipo hapa watachangia Sh milioni moja, nakukabidhi wewe (waziri mkuu) sasa hivi, utakabidhi kwa wafiwa hawa, kila mmoja atakaposimama… wameona wakuunge mkono ili kazi iende vizuri,” amesema Chalamila.
Aidha, Waziri Mkuu amesema kamati za usimamizi wa maafa katika ngazi ya mkoa na halmashauri ambazo wakuu wa mikoa na wilaya ndio wenyeviti kamati hizo zilizoanzishwa kwa mujibu wa sheria ya usimamizi wa maafa ya mwaka 2022, zitaendelea kuimarishwa ili ziweze kuchukua hatua haraka maafa yatakapotokea katika maeneo yao.
Shughuli ya kuaga na kutoa heshima za mwisho zimefanyika katika uwanja wa Kaitaba kabla ya kukabidhiwa kwa ndugu kwa taratibu za kifamilia.
Ajali hiyo iliyokea baada ya ndege kuzama ndani ya maji ya Ziwa Victoria, hatua chache kutoka uwanja wa ndege wa Bukoba.
Leave a comment