RAIS Samia Suluhu Hassan leo Jumatatu ameagiza kijana Jackson Majaliwa, mvuvi wa Bukoba aliyewezesha uokozi wa abiria 24 wa ndege ya Precision Air Ziwa Victoria atafutiwe nafasi ya ajira kwenye Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.
Pia ameagiza mazishi ya wahanga wote 19 yagharimiwe na serikali hivyo wakuu wa mikoa katika maeneo husika wasimamie kikamilifu mazishi hayo.
Hayo yameelezwa leo tarehe 6 Novemba, 2022 na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati wa ibada maalum ya kitaifa ya kutoa heshima za mwisho kwa miili 19 waliofariki katika ajali hiyo iliyotokea jana Jumapili.
Amesema Rais Samia ambaye yupo kwenye ziara nchini China, amempigia simu na kuagiza akabidhiwa kwa Waziri wa Mambo ya Ndani (Hamad Masauni) atafutiwe nafasi kwenye jeshi la uokozi.
“Ili kijana huyu apate mafunzo zaidi ya ujasiri wake huo aingie kwenye jeshi hilo (Jeshi la Zimamoto na Uokoaji) ambalo linahitaji kijana jasiri kama aliouonesha kijana wetu,” amesema.
Aidha, Waziri mkuu amesema mbali na kufurahishwa na maelekezo hayo ya Rais Samia, naye kama mtendaji mkuu anamsisitiza waziri wa mambo ya ndani baada ya tukio hilo la kuaga miili hiyo akutane na kijana huyo ili apate taratibu za na anuani zake mara na kuenda jeshini.
Awali Mkuu wa mkoa wa Kagera, Albert Chalamila kwa niaba ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alimkabidhi kijana Sh milioni moja kutokana na ushujaawake aliouonesha na kufanikiwa kuokoa watu 24 waliokuwa kwenye ndege ya Precision Air iliyoanguka jana asubuhi kwenye Ziwa Victoria wilayani Bukoba mkoani Kagera.
Hata hivyo, kabla ya kumaliza hotuba yake, Majaliwa pia alitangaza kwamba, Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya Becco, Gurpal Bharyan ametoa Sh milioni tatu kwa kijana huyo mwokozi.
“Tunakushuru sana hii ni ishara njema kwamba lazima tutambue ujasiri wa kijana wetu,” amesema.
Leave a comment