KAMPUNI ya Vodacom Tanzania katika mwendelezo wake wa kuwajali wateja na watu wenye ulemavu, imezindua dawati maalum la huduma kwa wateja litakalohudumia watu wenye ulemavu wa macho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizindua huduma hiyo, Philip Besiimire, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, amesema kuwa Vodacom imezindua huduma hiyo kwa lengo la kuwasaidia walemavu wa macho ili kupata huduma sawa na watu wengine.
“Leo tunazindua huduma hii mahususi kwa wateja wetu ambao wana changamoto ya uoni ili wapate huduma sawa na wateja wengine,” amesema Besiimire.
Amesema mbali na dawati hilo Vodacom imesema imewapa mafunzo maalum watoa huduma wao ili kutoa huduma hizo.
Thadayo Ringo, Meneja wa Masuala ya Wateja na Watumiaji Huduma za Mawasiliano kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ameesema Vodacom wanazidi kufanya vizuri kwenye utoaji wa huduma na kujali wateja ambao ndiyo wadau muhimu kwenye sekta ya mawasiliano.
“Vodacom imeonyesha kwa vitendo kuwajali watumiaji, hatua waliochukua ni hatua za awali za kuhakikisha kuwa hakuna anayechwa kwenye uchimi wa kidogitali,” amesema Ringo.
Habib Mlope, Mkurugenzi wa Kituo cha Sanaa na Utamaduni kwa Viziwi, amewapongeza Vodacom kwa kuendelea kutoa huduma kwa watu wenye ulemavu na kwamba inaboresha mawasiliano.
“Kabla ya huduma hii, Vodacom walizindua huduma kwa ajili ya viziwi kwenye lugha ya alama sasa maduka ya Vodacom mbalimbali kunatolewa huduma kwa lugha ya alama kwa ajili ya watu wasiona,” amesema Mlope.
Habiba Ngulangwa, Mwenyekiti wa Chama cha Watu Wasioona Tanzania, ameshukuru Vodacom kwa kubuni huduma inayowapa fursa ya kutumia simu kwa faragha na kupata dawati la kipekee la kusikilizwa.
“Tumeona hapa jinsi teknolojia hii itakayomwezesha mtu yoyote asiyeona hata akiwa kijijini anaweza kujihudumia yeye mwenyewe bila kuhitaji msaada,” amesema Ngulangwa.
Amesema kuwa atawahamasisha wanachama wote kutumia teknolojia hiyo ili kutumia mawasiliano kirahisi lakini pia kuhifadhi faragha zao.
Leave a comment