WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa amesema, tangu Serikali ya awamu ya tano ilipoingia madarakani tarehe 5 Novemba 2015, imefanikiwa kuanzisha viwanda 8,477 katika mikoa 26 ya Tanzania Bara. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea)
Kati ya viwanda hivyo vilivyoanzisha katika utawala huu unaoongozwa na Rais wa Tanzania John Magufuli, viwanda vikubwa ni 201, viwanda vya kati ni 460, vidogo ni 3,406 na viwanda vidogo sana ni 4,410.
Waziri Bashungwa amesema hayo leo tarehe 13 Mei 2020, wakati akijibu swali la Zacharia Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM).
Issaay ameuliza Je, ni lini Serikali itaanza kufanya tathmini ya mafanikio ya viwanda 100 kwa kila Wilaya ili kuchochea uchumi wa nchi yetu?
Akijibu swali hilo, Waziri Bashungwa amesema, Serikali ilifanya tathmini ya jumla ya upimaji wa mafanikio ya azma ya ujenzi wa viwanda Februari, 2020.
“Matokeo yalionesha kwamba, jumla ya viwanda 8,477 vimeanzishwa katika mikoa 26 ya Tanzania Bara tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani. Kati ya viwanda hivyo, viwanda vikubwa ni 201, viwanda vya kati ni 460 viwanda vidogo ni 3,406 na viwanda vidogo sana ni 4,410,” amesema Waziri Bashungwa
Amesema, vilevile wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais Tamisemi na Ofisi ya Taifa ya Takwimu, imeandaa mpango mahsusi wa kufanya tathmini pana ya viwanda vyote vilivyopo Tanzania Bara mwaka 2020/2021 kupitia zoezi maalum linalojulikana kama ‘Industrial Mapping’.
“Zoezi hilo litazingatia pia kufanya tathimini ya mpango wa viwanda 100 kila mkoa na litabainisha idadi na aina ya viwanda vilivyopo nchini; ajira, bidhaa zinazozalishwa, mapato; teknolojia zinazohitajika pamoja na malighafi zinazotumika ili uanzishwaji wa viwanda uendane pia na malighafi zinazopatikana hapa nchini ili kuwa na viwanda endelevu,” amesema
Waziri Bashungwa amesema wizara yake kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali za Serikali pamoja na sekta binafsi, inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuendeleza ujenzi wa viwanda ili azma ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati unaojengwa kupitia viwanda, iweze kufanikiwa ifikapo mwaka 2025.
Leave a comment