TAASISI ya Jakaya Mrisho Kikwete (JMKF) kwa kushirikiana na Asasi ya Umoja wa Mataifa (UNA) Tanzania na wadau mbalimbali imewakutanisha jumla ya vijana 150 katika mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kuimarisha biashara na kazi endelevu za mashirika ya vijana. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mafunzo hayo ambayo ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya Vijana duniani (IYD2022), yamefanyika leo tarehe 2 Septemba, 2022 jijini Dar es salaam.
Mafunzo hayo yanatarajiwa kuwa jukwaa la kufichua fursa na rasilimali kwa vijana ambazo zitasababisha kukuza upatikanaji wa kazi zenye staha na kukuza ushiriki wao bora kwenye masuala yanayowahusu.
Kitaifa maadhimisho haya yalifanyika tarehe 12 Agosti, 2022 na kaulimbiu ilikuwa “Kila mmoja anahusika kujenga Uchumi Imara, Ustawi Na Maendeleo Endelevu: Jiandae Kuhesabiwa.”
Mtendaji Mkuu wa JMKF, Vanessa Anyoti alisema mafunzo hayo yatafundishwa na wataalam waliobobea katika sekta binafsi na asasi za kiraia.
Alisema “Mafunzo haya ambayo yameandaliwa kwa pamoja na vijana, yatatumika kuchochea ujuzi na maarifa, ushauri kutoka kwa wabobezi katika sekta husika ili kuongoza mazungumzo baina ya vizazi. Maeneo ya mafunzo yaliyoainishwa katika programu yalipendekezwa na zaidi ya vijana 50 kutoka sekta binafsi na za kiraia.”
Anyoti aliongezea kwamba: “Siku ya Vijana Duniani imekuwa jukwaa muhimu la kuthamini mchango mkubwa wa vijana katika kuleta maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kiutamaduni. Tanzania inaungana na mataifa mengine Wanachama wa Umoja wa Mataifa kujadili, kusherehekea na kutambua nafasi ya Vijana katika kuleta maendeleo ya kiuchumi, kutoa mapendekezo na kuonesha uwezo wa vijana.
“Hii, inatokana na ukweli kwamba, vijana ndio kundi kubwa katika jamii yoyote ile. Vijana ndio wenye nguvu zaidi ya kufanya kazi, Vijana ni wabunifu, Vijana ndio chachu ya mabadiliko chanya katika jamii na Vijana ndio walinzi wa historia na warithi wa Mataifa yao”, alifafanua.
Leave a comment