JESHI la Polisi Mkoani wa Shinyanga nchini Tanzania, linachunguza ili kumkamata mwanamke anayetuhumiwa kujifungua watoto pacha kisha kuwatupa jalalani eneo la Kambarage mjini hapa. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana Jumatatu, tarehe 14 Machi 2022 na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, George Kyando tukio hilo linahisiwa kutendeka usiku wa kuamkia jana, ambapo mwanamke huyo ambaye hajafahamika, alivitupa vichanga hivyo na kutoweka.
Kamanda Kyando alisema Polisi inachunguza kwa kina ili kumbaini mtuhumiwa ili akamatwe na kufikishwa mahakamani kujibu mashitaka ya kutupa watoto aliojifungua.
“Ni kweli taarifa za tukio hilo tunalo, na tayari tumeelekeza kufanyika uchunguzi wa kina, ili kumbaini na kumkamata mtu aliyetenda kitendo hicho kiovu, ili achukuliwe hatua za kisheria,” alieleza Kamanda Kyando.
Baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo walielezea masikitiko yao juu ya unyama uliotendwa na mwanamke mzazi wa watoto hao na kuviomba vyombo vya Dola kumsaka na kumkamata, ili achukuliwe hatua kali za kisheria.
Mwenyekiti wa Mtaa wa Majengo mjini hapa, Majid Issa alisema tukio hilo ni la pili kutokea kwenye jalala hilo, na kuviomba vyombo vya Dola kumsaka mhusika ili achukuliwe hatua za kisheria, huku akionya pia wanawake kuacha kufanya unyama huo.
“Tukio hili ni la pili kutokea katika jalala hili, kitendo kilichofanyika ni cha kinyama, binafsi nitoe mwito kwa wanawake waache ukatili kama huu, hata kama mtu mwenye mimba ameikataa, wavumilie wakijifungua wakabidhi watoto hao kwenye vituo vya malezi ya watoto wasio na wazazi badala ya kuwatupa,” aliasa Majid.
Baadhi ya mashuhuda wanaoishi jirani na jalala hilo, walisema watu wanaookota vitu chakavu kwenye majalala, ndiyo walibaini kuwepo kwa vichanga hao na kupiga kelele zilizosababisha watu kukusanyika eneo la tukio kujionea kilichojiri.
“Ilikuwa saa 12 alfajiri, tulisikia kelele kutoka eneo hili la jalala tukawahi kufika kuona nini kimetokea, tulikuta hawa vijana wanaookota vitu vichakavu, tukawauliza kilichojiri.
“Walituonesha miili ya vichanga hao ikiwa kwenye mfuko ambao awali walidhani kuna vitu vya maana, na walipoufungua wakabaini miili ya watoto,” alieleza Costantine Samwel mkazi wa Kambarage.
Samwel alisema baada ya kubaini hali hiyo, taarifa zilitolewa kwa viongozi wa Serikali ya Mtaa ambao nao waliwasiliana na Jeshi la Polisi, askari walifika eneo la tukio na kuchukua miili ya vichanga hivyo kwa hatua zaidi za upelelezi
Leave a comment