UONGOZI wa Wanawake Tanzania (UWT) wametoa pongezi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Samia Suluhu Hassan kwa ubunifu wake wa kuzindua filamu ya Tanzania Royal Tour katika ukumbi wa Paramount, Los Angeles nchini Marekani. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 25 Aprili, 2022, Mwenyekiti wa UWT, Gaudensia Kabaka amesema safari za Rais Samia zimeonesha mafanikio makubwa.
Amesema Rais Samia amefanikiwa kuwatafuta wawekezaji wakubwa ambao watawekeza nchini kwa mitaji mikubwa.
“Tumeona katika ziara ya Rais pamoja na Mawaziri wake akiwemo waziri wa uwezeshaji wamefanya makubaliano na mwekezaji ambaye amekubali kuwekeza mtaji nchini Shilingi trilion 11 jambo ambalo amesema kuwa litafanya kuwepo kwa maendeleo kwa Taifa na maisha ya mtu mmoja mmoja.
Ameongeza kuwa ubunifu wa Rais Samia kwa kushirikiana na mwandishi nguli na mtengeneza filamu, ni kitendo cha kijasiri na ni historia ambayo haiwezi kufutika nchini na duniani.
Pia Kabaka amewahimiza watanzania kujenga utamaduni wa kufanya utalii wa ndani kwa maelezo kuwa watakuwa wamejifunza mengi na pia wataongeza pato la taifa.
Katika hatua nyingine, Kiongozi huyo wa UWT amesema kifo cha aliyekuwa mbunge wa Viti Maalum, Irene Ndyamukama (CCM) kutoka mkoa wa Rukwa, kimewashtua.
Amesema kifo hicho kimesababisha kukwama kwa malengo ya mbunge huyo ambayo alikuwa amejiwekea.
“Alikuwa ameanzisha ujenzi wa nyumba ya mtumishi mkoani Rukwa na alikuwa amepanga baada ya kujifungua atamalizia nyumba hiyo na kuweka vitu vyote vya thamani.
“Kutokana na hali hiyo natoa wito kwa yoyote atakayepata nafasi hiyo kuhakikisha anamalizia nyumba hiyo na kuweka samani zote na hiyo ndiyo itakuwa zawadi pekee ya kumuenzi,” amesema Kabaka.
Leave a comment