BILIONEA wa Nigeria, Aliko Dangote, anatarajiwa kuanza uwekezaji katika sekta ya sukari nchini Tanzania. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa jana Jumapili, tarehe 24 Aprili 2022, jijini New York nchini Marekani na Msemaji Mkuu wa Tanzania, Gerson Msigwa, katika mkutano wake na Watanzania waishio nchini humo, ambao umerushwa mubashara mitandaoni.
Msigwa alitoa kauli hiyo baada ya kuulizwa swali na Said Abdallah, mikakati ya Serikali katika kuwawekea mazingira bora wawekezaji nchini, akidai Dangote anapigwa vita kitendo kinachopelekea ashindwe kuzalisha saruji.
“Dangote hajapigwa vita, anaendelea kufanya kazi kama kawaida, anaendelea kuzalisha saruji. Amekuwa akipata changamoto za hapa na pale, za kawaida kuhusu uzalishaji lakini tumekuwa tukiwasiliana naye na sasa hivi anataka kupanua uzalishaji azalishe pia sukari na mengine mengi,” amesema Msigwa.
Msemaji huyo wa Serikali ya Tanzania, amesema Serikali inaendelea kushirikiana na Dangote, kwa kuwa ni mwekezaji wa kimkakati.
“Ni mwekezaji wa kimkakati na sisi kama Serikali tunaendelea kushirikiana na Dangote, hatuwezi kumpiga vita kwa namna yoyote sababu tunafahamu mchango anaoutoa kwenye nchi yetu,” amesema Msigwa.
Hivi karibuni, Serikali ya Tanzania imewakarribisha wawekezaji katika sekta mbalimbali hasa ya sukari, mbolea na mafuta ya kula, ili kuongeza upatikanaji wa bidhaa hizo muhimu nchini.
Leave a comment