KATIKA kujenga uwezo kwa kampuni ndogondogo zinazojishughulisha masuala ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Tume ya Tehama (ICTC) inatarajia kujenga vituo katika mikoa nane vitakavyokuwa na uwezo wa kuhudumia kampuni 270 zinazojishughulisha na TEHAMA. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Pia ICTC imepanga kupeleka nje ya nchi kampuni 10 kunolewa katika masuala ya TEHAMA ili washiriki wake watakaporejea nchini, wawe walimu kwa wenzao na pia wawe chachu ya kukua kwa masuala ya kidijitali nchini.
Hayo yameelezwa na Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Tehama (ICTC), Dk. Nkundwe Mwasaga wakati akizungumza na wajumbe wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) katika Mkutano Mkuu wa Saba wa Jukwaa hilo uliofanyika mjini Lindi wiki iliyopita.
Mkurugenzi mkuu huyo amesema vituo hivyo vitajengwa katika mikoa ya Lindi, Tanga, Mbeya, Arusha, Dodoma, Dar es Salaam, Mwanza na Zanzibar na lengo ni kujenga vituo katika mikoa yote na wilaya zote nchini, vitakavyowasaidia wananchi kuvitumia na kujifunza masuala ya teknolojia.
“Vituo hivyo vitajengwa maeneo yaliyo karibu na shule na vyuo ili viwasaidia vijana nchini kubuni na kuanzisha kampuni changa za ubunifu wa vitu mbalimbali,” alisema.
Aidha, Dk. Mwasaga alisema tume hiyo imejipanga kuhakikisha kila mtanzania anapata maarifa ya TEHAMA kidijitali ili aweze kuwa na maarifa zaidi ya kunufaika na sekta hiyo kwa sababu dunia ndiko ilikoelekea.
“Dunia sasa kila kitu kiko kwenye TEHAMA na sisi Tanzania kama sehemu ya dunia, mwaka 2015 Serikali ililazimika kuanzisha Tume ya Tehama ili pamoja na mambo mambo mengine, iwe na jukumu la kusimamia suala la mawasiliano kidijitali hapa nchini,” alisema.
Aidha, alisema tume hiyo ambayo majukumu yake ni pamoja na kutunga sera ya TEHAMA na kukuza TEHAMA, pia imelenga kuitangaza sekta hiyo na kuwajengea uwezo Watanzania kushiriki katika uchumi wa kidijitali.
Akifafanua sababu za kuanzishwa kwa tume hiyo mwaka 2015, Dk. Mwasaga alisema Serikali iliona njia pekee ya kuimarisha sekta ya TEHAMA ni kuwa na chombo maalum kitakachokuwa kikisimamia eneo hilo ili liwe na mafanikio zaidi, si kwa Tanzania pekee bali pia katika nyanja za kimataifa.
“Kutokana na umuhimu huo, ndiyo maana Serikali ikaamua kuanzisha tume hii ambayo ndiyo mlezi wa taasisi zote zinazohusika na masuala ya Tehama kama nilivyosema,” alisema.
Alisema katika kuhakikisha mapinduzi ya kidijitali yanafikiwa, ICTC imepanga kuhakikisha huduma mawasiliano zinawafikia watanzania wote bila ubaguzi kama vile ujenzi wa minara na kuihuisha kutoka 2G kwenda 4G na kuendelea.
“Pia kuhakikisha watanzania wanapata namba moja ya kidijitali ambayo inamtambulisha mtanzania mmoja. Namba hii inayoitwa ‘Jamii Namba’, itarahisisha upatikanaji wa huduma mbalimbali ikiwamo hata mikopo katika taasisi za kifedha.
Leave a comment