CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Taifa kimeitaka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuweka mfumo utakaotumika na kufanya msamaha wa Kodi kutokuwa kikwazo na kuchelewesha kuanza kwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini. Anaripoti Christina Haule, Ifakara … (endelea).
Hayo yalisemwa Jana na Katibu Mkuu CCM Taifa Daniel Chongolo wakati akiongea na wananchi katika mkutano wa hadhara kwenye kata ya Kiungani Wilayani Kilombero mkoani hapa.
“haiwezekani eti wenyewe tumesaini mkataba, lakini sisi wenyewe utubane na vikwazo vilivyokuwa wazi, tayari mradi ukishakuwa na neno msamaha wa kodi unapaswa kuzingatiwa ili kuharakishwa utekelezaji wa mradi, kuliko mradi kuchukua muda mrefu bila kuanza na kuacha wananchi wakiendelea kubaki na adha ya changamoto kama Serikali haijasikia kilimo chao,” alisema Chongolo.
Hivyo alisema lazima TRA iweke dirisha moja maalum la kushughulikia miradi yenye msamaha wa kodi ili kurahisisha utekelezaji wake.
Awali Kaimu Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) mkoani Morogoro, Mhandisi Sospeter Lutonja, alisema Serikali licha ya kutenga Sh. 42 bilioni ili kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama katikati vitongoji na vijiji Wilayani Kilombero mkoani hapa utekelezaji huo ulikwamishwa na taratibu za msamaha wa kodi.
Mhandisi Lutonja alisema Ifakara inakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa maji kutokana na wingi wa watu waliopo na kwamba Wilaya hiyo ingetakiwa kupata maji mili lita za ujazo mil 12 kwa siku lakini kwa sasa inapata lita 2.9 milioni kutokana na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi zinayotokana na shughuli mbalimbali za kibinadamu zinazofanywa ikiwemo ukataji wa miti hovyo.
Alisema usambazaji wa maji katika maeneo hayo unatakiwa kuwa wa miezi 20 ambapo ulitarajiwa kuwa umeshaanza na unatarajiwa kukamilika mwezi mei mwaka 2023.
“Mradi huo mpaka sasa ulitarajiwa kuwa tayari umeshaanza lakini mkandarasi hajaanza kwa ajili ya changamoto ya Utaratibu wa msamaha wa Kodi,” alisema Mhandisi Lutonja.
Hivyo alisema mradi huo unatarajia kunufaisha wananchi wapatao 129,000 na kuzalisha.lita za maji mil 20 kwa siku zitakazotumika na wananchi na kuwa na uhakika wa maji kwa miaka 20 ijayo yaani Hadi mwaka 2045.
Akizungumzia Jimbo la Mlimba, Mhandisi Lutonja alisema kwa sasa wananchi wa vijiji vya Mlimba wameanza kunufaika na mradi mkubwa wa maji uliopo kwenye Kijiji cha Kalengakero ambao unasambaza maji katika vijiji vyote vya wilaya hiyo.
Leave a comment