KATIBU mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa Daniel Chongolo ameiagiza kamati ya ulinzi na usalama Wilayani Malinyi mkoani Morogoro kuwasweka ndani watendaji wa vijiji na kata wanaoonyesha mianya ya rushwa inayosababisha migogoro ya wakulima na wafugaji ili kuondoa migogoro na kuimarisha amani ya nchi. Anaripoti Christina Haule, Malinyi … (endelea).
Chongolo alisema hayo wakati akizungumza kwenye mkutano na wananchi wa kijiji cha Itete Wilaya ya Malinyi mkoani Morogoro ambapo alisema wapo viongozi wenye tabia ya kupokea rushwa na kuruhusu mifugo iingie hata maeneo ambayo hayana nafasi ya mifugo.
Hivyo alisema chama hakitakuwa sehemu ya kuwakingia vifua wenyeviti wa vijiji na vitongoji watakaosababisha na kuchochea migogoro ya wakulima na wafugaji.
“Wapo viongozi wanaotumia madaraka yao vibaya, wanaruhusu mambo yasiyofaa kuendelea kutokea kwenye maeneo yao bila ya kujali athari zake za baadaye na athari zikishatokea uhisi kusaidiwa na chama hakitahusika wala hakitakinga kifua kwa yeyote atayehusika,” alisema Chongolo.
Alisema migogoro ya wakulima na wafugaji mara nyingi hutokea kwa sababu ya viongozi husika kutosimamia kanuni na taratibu zilizowekwa na pengine kuingia makubaliano na kujinufaisha wenyewe.
Hata hivyo aliagiza Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kuhakikisha ujenzi wa barabara ya Malinyi hadi Namtumbo mkoani Songea unaanza wiki mbili zijazo na kukamilika mapema ili kusaidia maendeleo kwa wakazi wa maeneo hayo sambamba na kuifanya Tanzania kuwa sehemu na kivutio cha utalii kwa kuwa na barabara nyingi za kiwango cha lami.
Naye katibu wa tawi shina namba 5, Geofrey Mgobole alisema kata hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya mifugo kuingia bila utaratibu na kuharibu mazao yao mashambani sambamba na kuharibu miundombinu.
Hivi KM wa CCM ana mamlaka gani juu ya watendaji wa serikali? Wao si wana mabosi wao?