KATIBU Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo, amesema vigingi vilivyowekwa kwenye misamaha ya kodi ndio kikwazo kikubwa kinachosababisha kuchelewa kukamilika kwa wakati baadhi ya miradi ya maendeleo na kimkakati inayoendelea kutekelezwa hapa nchini. Anaripoti Christina Haule, Kilombero … (endelea).
Amesema kutokana na changamoto hiyo, ipo haja ya kuwepo kwa dirisha moja ambalo litakuwa linawajibika na miradi inayoingia nchini ambayo inahitaji kutekelezwa kupitia msamaha wa kodi, hiyo ni baada ya kushindwa kukamilika kwa wakati ujenzi wa daraja la Ruaha Mkuu linalounganisha Mikumi na Kilombero kutokana na vikwazo vya msamaha wa kodi ya ongezeko la thamani VAT.
Chongolo ametoa kauli hiyo wakati akiwa Ifakara, wilayani Kilombero mkoani Morogoro ikiwa ni muendelezo wa ziara yake ya siku tisa inayolenga kukagua utekelezaji wa ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020-2025 pamoja na kuzungumza na makundi mbali mbali ya kijamii.
“Serikali ni moja, msamaha wa kodi tunatoa wenyewe, mradi tuna sainisha wenyewe, halafu jambo moja la msamaha wa kodi linakuwa nyuma wakati la kusaini mradi linakuwa mbele, ninadhani ifike mwisho na isiwe hoja tena kwa wananchi” amesema Chongolo.
Chongolo ameongeza kuwa kuanzia sasa Serikali inapaswa kuweka mfumo wa kuhakikisha msamaha wa kodi hauwi kikwazo tena kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
“Mpaka inaitwa msamaha wa kodi maana yake ndani ya Serikali kumechakatwa mradi, tukakubaliana kwamba mradi utatekelezwa kwa kuondosha kodi na hasa ya Ongezeko la Thamani, kwa hiyo lazima twende tukashughulike na hilo” amesisitiza Chongolo.
Leave a comment