Tanzania na Zambia zimekubaliana kutatua changamoto nane kati ya 24 za kibiashara na 16 zilizobaki zimewekewa utaratibu wa kuzitatua ifikapo tarehe 31 Disemba 2023 ili kurahisisha ufanyajibiashara baina ya nchi hizo ikiwemo kupunguza msongamano wa malori katika mpaka wa Tunduma. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Dk. Hashil Abdallah juzi Jumatano wakati akizungumza na vyombo vya habari baada ya Mkutano wa Pamoja wa Kujadili Changamoto za Biashara kati ya Tanzania na Zambia uliofanyika tarehe 9 na 10 mwezi huu katika Kituo cha Huduma za Pamoja Mpakani- Tunduma, Songwe.
Aidha, Dk. Abdallah amesema nchi hizo zimekubaliana kuwa bidhaa zinazosafirishwa kutoka Tanzania kwenda nchi nyingine kupitia Zambia zikiwa na vibali vyote vinavyohitajika ziruhusiwe kupita nchini humo kwenda nchi husika bila kizuizi kulingana na Makubaliano ya Kibiashara chini ya Shirika la Biashara la Dunia (WTO) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).
Vilevile, amezitaka Taasisi zote za umma zinazohusika na utoaji wa huduma kwa wafanyabiashara wa huduma ya usafirishaji baina ya nchi hizo kuhakikisha hawawakwamishi bila sababu za msingi bali kuwasaidia kutatua changamoto zao hususani upatikanaji wa vibali kulingana na Sheria, Kanuni na Taratibu zilizopo katika makubaliano ya kibiashara chini ya Shirika la Biashara la Dunia na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika.
Katika kuhakikisha masuala hayo yanafanikiwa, Dk. Abdallah ametoa rai kwa wafanyabiashara ya usafirishaji wa bidhaa mbalimbali kuhakikisha wanapata vibali vyote vinavyohusika kabla ya kuanza safari ili kurahisisha usafirishaji wa bidhaa hizo bila vikwazo na kuzifikisha katika nchi husika kwa wakati.
Katika hatua nyingine ya makubaliano yaliyotiwa saini na pande zote mbili, amesema Serikali ya Tanzania imekubali kufanya mapitio na marekebisho ya Tozo ya Maendeleo ya Reli kama inavyotekelezwa katika Itifaki ya Biashara ya SADC na kuharakisha mchakato wa urazinishaji wa kanuni za usafirishaji ili ziendane na kanuni za usafirishaji zinazotekelezwa katika Eneo Huru la Biashara la Utatu (Tripatite transport regulations).
Kwa upande wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara na Viwanda Zambia, Lillian Bwalya amesema nchi ya Zambia imekubali kutatua changamoto hizo ili kurahisisha na kukuza biashara za mpakani baina ya nchi hizo.
Akitaja baadhi ya makubaliano yaliyotiwa saini baina ya nchi hizo, amesema Zambia imekubali kuboresha changamoto za miundombinu ikiwemo upanuzi wa barabara na kutekeleza mfumo wa upatitanaji wa vibali kabla ya kufika mpakani ili kuboresha mtiririko wa magari mpakani na kuondoa msongamano wa magari uliopo mpakani Tunduma.
Aidha, amesema Zambia imekubali kutumia mfumo wa ufuatiliaji wa mizigo kwa njia ya elektroniki unaotekelezwa nchini Tanzania, au kuharakisha mchakato wa ununuzi wa mfumo unaopendekezwa kutumiwa na Mamlaka ya Mapato ya Zambia (ZRA).
Vilevile, Zambia imekubali kuharakisha urazinishaji wa ada na tozo za barabara kwa Dola za Marekani 10 kwa kilomita 100 unaotekelezwa kaitika Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC).
Bwalya pia amesema Zambia imekubali kuangalia uwezekano wa kutumia mfumo wa kisasa wa ufuatiliaji wa magari barabarani ili kuondoa na kupunguza vizuizi vya ukaguzi barabarani.
Vilevile, Zambia imekubali kutumia Ofisi jijini Dar es Salaam inayotolewa na Serikali ya Tanzania kwa ajili ya Maafisa wa uondoshaji wa mizigo ya Zambia kuanzia Desemba 31, 2023 ili kirahisisha usafirishaji wa mizigo na kuondoa msongamano wa magari mpakani.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi Prof. Godius Kahyarara amesema makubaliano hayo ni muhimu katika kutatua changamoto mbalimnali baina ya nchi hizo hususani katika kupunguza msongamano wa malori katika mpaka wa Tunduma unaopitisha asilimia 80 ya mizigo kutoka Bandari ya Dar es salaam kwenda nchi za kusini mwa Afrika zisizo na bahari.
Kwa upande wa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha (Usimamizi na Uchumi), Elijah Mwandumbya akishiriki mkitano huo amesema tozo na kodi mbalimbali zitaendelea kupitiwa na kurekebishwa ili kuwezesha sekta binafsi kutumia fursa mbalimbali zinazojitokeza kutokana na makubaliano hayo ili kukuza biashara na uchumi wa Taifa
Naye Balozi wa Tanzania nchini Zambia, Luteni Jenerali Mathew Edward Mkingule amesema changamoto zilizoondolewa zitaongeza ufanisi wa utoaji huduma na kukuza ushirikiano wa kibiashara baina ya nchi hizo.
Leave a comment