Thursday , 2 May 2024
Home Habari Mchanganyiko Serikali yatakiwa kutunga sheria kudhibiti ajali mabasi ya shule
Habari Mchanganyiko

Serikali yatakiwa kutunga sheria kudhibiti ajali mabasi ya shule

Spread the love

KUFUATIA ajali ya basi la shule ya msingi ya Ghati Memorial, iliyogharimu maisha ya wanafunzi nane, Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), umeishauri Serikali itunge sheria na sera kali zitakazosaidia kutokomeza ajali hizo zinazosababishwa na uzembe. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).

Akizungumza na MwanaHALISI Online, Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, amesema baadhi ya  watoto wamekuwa wakikabiliwa na vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu kama vile kupoteza maisha kwa ajali za kizembe na hata kubakwa na kulawitiwa, kwa kuwa hakuna sera na sheria zinazowabana wamiliki wa shule kuajiri watu wenye sifa sahihi za kuhudumia watoto.

“Sasa tumeona anachukuliwa dereva, mtumishi na mwalimu hana mafunzo yoyote ya mtoto, hana nidhamu ya kukaa na mtoto mwisho wa siku ndio haya yanayotokea madereva wanaua watoto, wanabaka watoto na matukio mengi yanakwenda kuwadhalilisha watoto tunapaswa kuwalinda watoto,” amesema Olengurumwa.

Olengurumwa amesema “sisi watetezi wa haki za binadamu tunaishauri Serikali ije na sheria na sera za kuwalinda watoto wanapokuwa katika mikono ya taasisi hizo, ili tuhakikishe tunaweka mazingira salama ya kukua na kupata maarifa kwa ajili ya taifa la kesho.”

Olengurumwa amesema sheria na sera zikitungwa zitaweka utaratibu juu ya namna ya kupata watumishi wa shule wanaofaa na wanaozingatia sheria, badala ya hali iliyopo sasa ambapo mmiliki anaajiri mtu yeyote hata kama hana mafunzo juu ya namna ya kulea na kuhudumia watoto.

“Tunapoangalia malezi ya watoto tuangalie zile taasisi zinazohusiana na malezi tumeweka kanuni na sheria zipi kuzisimamia? Kuanzia tunavyoweza kuwapata watumishi wake, walimu, madereva na wengine. Tuna utaratibu gani tunaotumia kuwapata? Je, tunawapa mafunzo gani kuhusiana na usimamizi na ulinzi wa mtoto? nasisitiza tuwe na utaratibu mzuri wa kuwapata watumishi,” amesema Olengurumwa.

Ajali hiyo iliyokea mwishoni mwa wiki iliyopita, ambapo chanzo kinadaiwa ni uzembe wa dereva aliyelazimisha kutaka kupita katika maji yanayokwenda kasi, kisha basi kutumbukizwa korongoni.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

BiasharaHabari Mchanganyiko

NMB yang’ara maonesho OSHA

Spread the loveBenki ya NMB imebeba tuzo ya kampuni bora kwenye sekta...

Habari MchanganyikoKimataifa

Ruto amteua Kahariri kuwa mkuu wa majeshi

Spread the loveRAIS wa Kenya, William Ruto, amemteua Jenerali Charles Muriu Kahariri,...

Habari Mchanganyiko

Chongolo aonya viongozi vijiji kutouza NIDA kwa wageni

Spread the loveMKUU wa Mkoa wa Songwe, Daniel Chongolo amewaonya viongozi wa...

Habari Mchanganyiko

TUCTA, OSHA wataka kampuni za madini kuiga ubunifu wa GGML

Spread the loveSHIRIKISHO la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) pamoja na Wakala...

error: Content is protected !!