SERIKALI ina mpango wa kujenga bandari ya uvuvi wilayani Bagamoyo, ili kuimarisha shughuli za uchumi wa buluu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo ameyasema Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 19 Septemba 2023, akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa mradi wa Bandari ya uvuvi unaogharimu Sh. 266 bilioni na ugawaji boti za kisasa kwa wavuvi, Kilwa Masoko mkoani Lindi.
Amesema bandari hiyo itajengwa pale uchumi wa nchi utakaporuhusu, huku akiweka wazi mpango wa Serikali yake ya kuanzisha maeneo ya ufugaji samaki katika ukanda wa pwani ya bahari.
“Kutokana na ukubwa wa ukanda wa Pwani, tunafikiria pia bandari hii niliyoiona na maboto yanavyoletwa na mradi huu, tunataka kuanzisha maeneo ya ufugaji samaki na bandari hii inaweza ikatosha upande huu. Sababu ukanda wetu wa bandari ni mkubwa tunafikiria kujenga bandari nyingine ya uvuvi pale Bagamoyo hali ya uchumi ikituruhusu,” amesema Rais Samia.
Akizungumzia ujenzi wa Bandari ya Uvuvi Kilwa, Rais Samia amesema ukikamilika utasaidia kutoa ajira zaidi ya 20,000 na kutoa fursa mbalimbali ikiwemo za biashara kwa wananchi wa eneo hilo.
Kuhusu boti za kisasa zilizogawiwa kwa wavuvi, Rais Samia amewataka kurejesha kwa wakati mikopo hiyoili nyingine zinunuliwe kwa ajili ya kuwanufaisha wavuvi wengine.
Aidha, Rais Samia amewataka vijana kuchangia fursa za uvuvi ikiwemo kufuga samaki kwa kuwa masoko ya uhakika yapo.
Leave a comment