RAIS Samia Suluhu Hassan ameeleza kupokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha Waziri Mkuu Mstaafu, Edward Ngoyai Lowassa (70) aliyefariki leo Jumamosi saa nane mchana katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete Jijini (JKCI) Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Kupitia akaunti yake ya mtandao wa X (twitter), Rais Samia ameandika; “Lowassa ameitumikia nchi yetu katika nafasi mbalimbali kwa zaidi ya miaka 35, akianzia ushiriki wake katika Jeshi la Wananchi wa Tanzania, Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mbunge, Waziri katika wizara mbalimbali na Waziri Mkuu.
“Tumempoteza kiongozi mahiri, aliyejituma na kujitoa kwa nchi yetu. Natoa pole kwa mjane, Mama Regina Lowassa, watoto (Mheshimiwa Mbunge wa Monduli, Fredrick Lowassa na wadogo zako), ndugu, jamaa, marafiki na Watanzania wote kwa msiba huu mzito.
“Katika mawasiliano yangu na familia, nimewaeleza kuwa kama taifa tuko pamoja nao katika kipindi hiki kigumu, na kamwe wasiache kumtegemea Mwenyezi Mungu na kutafakari neno lake, hasa Kitabu cha Ayubu 1:21. Mwenyezi Mungu amweke mahali pema. Amina,” ameandika Rais Samia.
Kifo cha Lowassa kimetangazwa leo Makamu wa Rais Dk. Philip Mpango kwa niaba ya Rais Samia kupitia televisheni ya Taifa (TBC).
Amesema Lowassa alikuwa akipatiwa matibabu ya ugonjwa wa kujikunja utumbo, matatizo ya mapafu na shinikizo la damu.
Leave a comment