DAKTARI Ali Shein, Rais wa Serikali za Mapinduzi Zanzibar (SMZ), leo Jumamosi tarehe 20 Juni 2020 amelivunja Baraza la tisa la Wawawakilishi la Zanzibar. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Akizungumza wakati anavunja baraza hilo, Rais Shein amepongeza uongozi wa baraza hilo kwa kazi nzuri uliyoifanya, kwa ajili ya kuleta maendeleo ya Zanzibar.
Rais Shein amesema katika kipindi cha miaka mitano, baraza hilo limefanya kazi kubwa ya kuwatumikia wananchi, ikiwemo kupitisha bajeti za serikali na kutunga sheria mbalimbali.
“Nawapongeza kwa kazi nzuri mlizofanya, mlijadili nyaraka mbalimbali na mkachangia nyaraka hizo na kakubali hoja na maudhui yaliyoko kwenye nyaraka hizo, pamoja na kukubali bajeti zote, hongereni sana kwa kazi nzuri mlizofanya,” amesema Rais Shein na kuongeza.
“Mmekuwa mbele kwa masilahi ya wananchi kwa kutambua sote tunawajibika kwao, hapana shaka wananchi wameridhishwa na kazi mliyofanya na wana imani kwenu kama baraza la kutunga sheria.”
Rais Shein anamalizia kipindi chake cha mihula miwili ya uongozi (2010/2015 na 2015/2020), ambapo aliingia madarakani mwaka 2010.
Chama cha Mapinduzi (CCM) ambako Rais Shein anatoka kimeanza maandalizi ya uchaguzi kwa ajili ya kumpata mgombea wa urais atakayerithi mikoba yake kama atashinda kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020 .
Hadi sasa makada mbalimbali wameanza kujitokeza kuchukua fomu kwa ajili ya kugombea urais wa Zanzibar, kupitia CCM.
Leave a comment