UTAFITI wa Benki ya Stanbic umebaini kuwa mradi wa kuchakata gesi asilia (LNG) uliofufuliwa na Rais Samia Suluhu Hassan utaingiza zaidi ya dola za Marekani bilioni 7 kwa mwaka (sawa na Shilingi trilioni 16.5) kwenye Pato la Taifa (GDP). Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Utafiti huo huru wa Benki ya Stanbic uliozinduliwa leo tarehe 26 Oktoba, 2022 jijini Dar es Salaam umeweka wazi kuwa mradi huo wa LNG utaleta mageuzi makubwa kwenye uchumi wa Tanzania.
“Zao Ghafi la Ndani linatarajiwa kwa ongezeko la kila mwaka kwa Dola za Marekani Bilioni 7 hadi kufikia Dola za Kimarekani Bilioni 15,” ilisema ripoti hiyo.
“Mradi utanufaisha upatikanaji wa mtaji wa taifa kwa kiwango cha mwaka cha Dola za Kimarekani Bilioni 50.”
Tangu alipoingia madarakani Machi 2021, Rais Samia alitangaza kutoa kipaumbele kikubwa kwa mradi huo wa LNG ambao ulikwama katika serikali za awamu za 4 na 5.
Rais Samia alifanya mabadiliko ya uongozi kwenye Wizara ya Nishati na kuagiza kuwa mazungumzo ya mradi huo kati ya serikali na wawekezaji wa nje yaharakishwe.
Kufuatia maagizo hayo ya Rais Samia, serikali inatarajia kusaini mkataba mkubwa wa ujenzi wa LNG na wawekezaji wa nje kabla ya mwisho wa mwaka huu.
Majadiliano rasmi kati ya serikali ya Samia na wawekezaji yalianza Novemba 2021 na yamekua yanaendelea kwa kasi jijini Arusha hadi sasa ili kukamilisha mradi huo.
Makampuni ya Equinor, Shell, Exxon Mobil na Ophir yanatarajia kujenga mtambo wa LNG mkoani Lindi kwa gharama za dola za Marekani bilioni 30 hadi 40.
Leave a comment