RAIS Samia Suluhu Hassan amewapongeza watafiti wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) kwa kazi kubwa za utafiti wanazofanya ambazo zinakuza sekta ya kilimo nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mbeya… (endelea).
Pongezi hizo amezitoa leo tarehe 8 Agosti, 2022 baada ya kupata maelezo kutoka kwa Waziri wa Kilimo Hussein Bashe, wakati Rais Samia alipotembelea banda la Wizara ya Kilimo, katika kilele cha Maonesho ya Kitaifa ya Wakulima yanayofanyika Viwanja vya John Mwakangale, jijini Mbeya.
Maonesho hayo ya mwaka huu yamebeba kauli mbiu ya Ajenda 10/30 Kilimo ni Biashara.
Waziri Bashe amemueleza Rais Samia kuwa Wizara inajenga uwezo wa Taasisi ya TARI kupitia Kituo cha Mlingano ili kufanikisha ukusanyaji wa sampuli za udongo nchi nzima na kuzipima katika maabara ili kubainisha afya ya udongo na kuwashauri wakulima juu ya watumizi ya mbolea ili kuzalisha kwa tija.
Kuhusu kukabiliana na uhaba wa mafuta ya kula, Waziri wa Kilimo Bashe, amemueleza Rais Samia kuwa Wizara kupitia taasisi za TARI, ASA na TOSCI itazalisha mbegu bora za alizeti tani 5,000 ambazo zitasambazwa kwa wakulima.
“Hatua hiyo itawawezesha wakulima kuzalisha alizeti nyingi ambayo itakamuliwa na kuongeza upatikanaji wa mafuta ya kula nchini,” amesema.
Akizungumzia utafiti, Bashe alimweliza Rais kuwa Serikali yake imeongeza bajeti ya utafiti kutoka shilingi bilion 11 hadi bilioni 40 kwa mwaka wa fedha wa 2022/23.
Amesema fedha hizo zitatumika kuongeza upatikanaji wa mbegu bora kwa mzao mbalimbali nchini.
Akizungumzia upatikanaji wa Mbegu bora za Mahindi Waziri Bashe alimweleza Rais Samia kuwa Wizara inaweka nguvu kuhakikisha mbegu bora ya mahindi ambayo ni chotara UH6303 inayofaa kwa ukanda wa Nyanda za Juu Kusini itazalishwa kwa wingi ili iweze kusambazwa katika ukanda huo.
Waziri amesema jitihada zinaendelea kuhakikisha mbegu bora zilizofanyiwa utafiti na TARI zinazalishwa na ASA ili ziweze kupatikana kwa wakulima.
Waziri Bashe pia alimjulisha Rais Samia kuwa, ili kuwa na vyanzo vya nasaba za utafiti wakati wot, Wizara imeanza kukusanya na kuhifadhi mbegu za asili ili zisipotee kwa matumizi ya sasa na ya baadae.
Katika ziara hiyo Rais Samia alitaka kujua kwamba upo uwezekano wa kuongeza ukubwa wa mbegu za alizeti ili mavuno kuwa mengi ambapo Mratibu wa zao hilo Kitaifa, Frank Ruben alimuhakikishia Rais kuwa inawezekana.
Alisema mbegu hizo inawezekana kuongeza au kupunguza ila kitakachotokea ni punje kwenye gunia kuingia chache kuliko zenye punje ndogo.
“Punje ndogo zitatoa lita 25 za mafuta kwa gunia la kilo 60 na punje kumbwa zitatoa lita 22 kwa gunia hilo Hilo,”alisema Ruben.
Leave a comment