RAIS wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameteua makatibu wakuu wanne, wa wizara na taasisi mbalimbali visiwani humo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa ya uteuzi huo imetolewa leo Ijumaa, tarehe 30 Julai 2021 na Katibu Mkuu Kiongozi Zanzibar, Mhandisi Zena Said.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Rais Mwinyi amemteua Dk. Fatma Mrisho, kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee, Jinsia na Watoto. Huku Khadija Khamis Rajab, akiteuliwa kuwa Katibu Mkuu, anayeshughulikia masuala ya kazi na uwezeshaji, katika Ofisi ya Rais, Kazi, Uchumi na Uwezeshaji.
“Dk. Habiba Hassan Omar, ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu anayeshughulikia masuala ya uchumi na uwekezaji, katika Ofisi ya Rais, Kazi, Uchumi na Uwekezaji,” imesema taarifa hiyo.
Dk. Omar Dadi Shajak, ameteuliwa na Rais Mwinyi kuwa, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, visiwani humo.
Taarifa ya Mhandisi Zena imesema kuwa, wateule hao wataapishwa Jumatatu, tarehe 2 Agosti 2021, Ikulu visiwani Zanzibar.
Pia, taarifa hiyo imesema, siku hiyo Rais Mwinyi atamuapisha Khamis Kona Khamis, aliyemteua kuwa Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC). Khamis aliteuliwa kushika wadhifa huo tarehe 16 Julai mwaka huu.
Leave a comment