KAMATI Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), imeelekeza makada wake wanaokiuka mienendo na maadili ya chama hicho, wachukuliwe hatua za kinidhamu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa tarehe 29 Julai 2021 na Katibu wa Itikadi na Uenezi CCM, Shaka Hamdu Shaka, akitoa maazimio ya kikao maalumu cha kamati hiyo, kilichofanyika jana jijini Dar es Salaam.
Shaka alisema, kamati hiyo imeeleza wanachama hao waanze kuchukuliwa hatua, kwa mujibu wa katiba ya CCM.
“Kamati Kuu imeeleza kuanza kuchukuliwa hatua kwa wale wote wanaokiuka mienendo, taratibu na kanuni za maadilina uongozi kwa mujibu wa katiba ya chama,” alisema Shaka.
Malekezo ya kamati hiyo yamekuja katika kipindi ambacho kuna mvutano kati ya Mbunge wa Kawe (CCM), Askofu Josephat Gwajima na Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan, kuhusu mpango wa kuwachanja wananchi chanjo ya Ugonjwa wa Korona (UVIKO-19).
Hivi karibuni, Askofu Gwajima alitangaza hadharani kupinga mpango huo, kwa madai kuwa una madhara kwa afya za Watanzania.
Hata hivyo, Serikali imekanusha madai hayo ikisema kwamba chanjo hizo ni salama.
Leave a comment