RAIS Mstaafu, Dk. Jakaya Kikwete, amesema amepokea kwa mshtuko kifo cha aliyekuwa Rais wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi, kwa kuwa alikuwa ana mchango mkubwa katika safari yake ya kisiasa na uongozi serikalini. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza wakati alipofika kuhani katika msiba wa Mzee Mwinyi, nyumbani kwake Mikocheni jijini Dar es Salaam, leo tarehe 1 Machi 2024, Kikwete amesema anamshukuru kwa kuwa alikuwa wa kwanza kubaini uwezo wake kisha kumpa nafasi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na hata kumshika mkono kwenye safari yake ya urais.
“Kwangu mimi binafsi ni shukrani maalum kwa sababu yeye ndiye aliyebaini uwezo wangu. Nilikuwa katibu wa CCM wa Masasi nimetokea kwenye Jeshi amenipeleka Nachingwea nikahamishiwa Masasi, pale Masasi ndiyo akaniteuya mbunge na naibu waziri na baada ya pale safari yangu ya mpaka kufikia kwenye urais,” amesema Dk. Kikwete.
Amesema “safari ndipo ilipoanzia pale, imeanza mikononi mwake kwa hiyo sina namna ya kusema kwamba , kwa kweli nimefika hapa nilipofikia kwa sababu yake yeye.”
Dk. Kikwete amesema taifa limepoteza kiongozi mzalendo aliyelipigania kwa dhati na kuleta mageuzi ya kiuchumi na kisiasa.
“Ameliongoza taifa letu vizuri, amepokea katika mazingira magumu lakini ameweza kuendesha nchi. Yeye ndiyo muasisi wa mageuzi. Mageuzi kwanza ya kiuchumi lakini baadae mageuzi ya kisiasa na sisi wengine wote tuliofuata tulikuwa tunafuata nyayo ya pale alipoachia yeye,” amesema Dk. Kikwete.
Rais Mwinyi aliyeiongoza Tanzania kuanzia 1985 hadi 1995, amefariki dunia tarehe 29 Februari mwaka huu katika Hospitali ya Mzena, alikokuwa anapatiwa matibabu ya saratani ya mapafu. Mwili wake utazikwa kesho Jumamosi, Mangapwani, Unguja visiwani Zanzibar.
Kiongozi huyo amefariki dunia ikiwa imesalia miezi michache atimize umri wa miaka 99, ambapo alizaliwa tarehe 8 Mei 1925.
Leave a comment