RAIS wa Hungary, Katalin Novak anatarajiwa kufanya ziara ya kikazi ya siku nne nchini kwa lengo la kuimarisha mahusiano ya mataifa hayo mawili. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa iliyotolewa leo Jumatatu na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk. Stergomena Tax, imesema ziara ya Rais Novak, itaanza tarehe 17 hadi 20, Julai 2023.
“Ziara hii ni matokeo ya jitihada za Rais Samia kuimarisha uhusiano wa Tanzania na mataifa mengine. Aidha, ziara hiyo inakuja kutokana na sera mpya ya Hungary kwa nchi za Afrika inayolenga kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, iliyoanza kutekelezwa miaka michache iliyopita,” imesema taarifa ya Dk. Tax.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Rais Novak atawasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, kisha kupokewa na Dk. Tax, kisha kesho atakwenda Ikulu jijini Dar es Salaam, kuzungumza na Rais Samia Suluhu Hassan.
“Watashiriki mazungumzo ya faragha na baadae mazungumzo rasmi. Baada ya mazungumzo watazungumza na waandishi wa habari, baadae kushiriki dhifa ya chakula Cha mchana. Siku hiyo pia atatembelea Ofisi ya ubalozi wa heshima ya Hungary,” imesema taarifa hiyo.
Ratiba iliyotolewa na Dk. Tax kuhusu ziara hiyo, imesema tarehe 19 Julai 2023, Rais Novak atakwenda jijini Arusha, kwa ziara binafsi na ataondoka kurejea Hungary kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro, tarehe 20 Julai mwaka huu
Leave a comment