JESHI la Polisi mkoani Mbeya, limemwachia Wakili Boniface Mwabukusi, baada ya kumshikilia kwa saa kadhaa tangu alivyoitikia wito wa kuripoti ili kuhojiwa dhidi ya tuhuma zilizokuwa zinamkabili. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mbeya … (endelea).
Taarifa za tukio hilo zimetolewa na Wakili Peter Madeleka, aliyedai kuwa, Jeshi la Polisi baada ya kumhoji Wakili Mwabukusi dhidi ya tuhuma zilizokuwa zinamkabili, wamemwachia huru bila kutaja sababu za kumkamata.
Mtandao huu umejitahidi kumtafuta Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya,Benjamin Kuzaga, kwa ajili ya ufafanuzi zaidi juu ya tukio hilo, lakini simu yake iliita bila kupokewa.
Kabla ya Wakili Mwabukusi kukamatwa, juzi Jumapili, Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Mkoa wa Mbeya,ACP Andrew Kantimbo, alimwandikia barua ya wito akimtaka afike ofisini kwake jana Jumatatu,kwa ajili ya kuhojiwa dhidi ya tuhuma hizo.
Inadaiwa kuwa, Wakili Mwabukusi na wenzake walifanya kusanyiko lisilo halali tarehe 8 Oktoba 2023, kwenye Kijiji cha Kandete, wilaya ya Busokelo, mkoani Mbeya.
Hii si mara ya kwanza kwa Wakili Mwabukusi kukamatwa na Jeshi la Polisi, kwani alishawahi kushikiliwa na jeshi hilo akituhumiwa kwa makosa mbalimbali, kufuatia msimamo wake wa kupinga mkataba wa uwekezaji bandarini, pamoja na madai ya upatikanaji wa katiba mpya.
Kupitia mwamvuli wa Sauti ya Watanzania, Mwabukusi na wenzake akiwemo Mdude Nyagali na Dk. Wilbroad Slaa, wametangaza kufanya maandamano tarehe 9 Novemba mwaka huu, kuishinikiza Serikali ivunje mkataba wa bandari kwa madai kuwa hauna maslahi kwa taifa.
Leave a comment