BENKI ya NMB nchini Tanzania imeendealea kuhamashisha wananchi na wafanyabiashara wa Kanda ya Ziwa kuchangamkia mikopo mbalimbali ikiwemo ya boti za uvuvi ili kuchangia ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla, kupitia sekta ya uvuvi. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Mkuu wa Idara ya Biashara wa Benki hiyo, Alex Mgeni alitoa rai hiyo mwishoni mwa wiki wakati wa mkutano wa Mtandao thatibiti kwa ukuaji endelevu wa biashara.
Mkutano huo uliandaliwa na NMB na kuwakutanisha wafanyabiashara wakubwa wa mkoa wa Mwanza, kujadili masuala mbalimbali, ikiwemo upatikanaji rahisi wa mikopo ya Benki hiyo, kwa ustawi wa biashara zao.
“Tumeshatoa mikopo ya aina hii Zanzibar kwa ajili ya uvuvi na utalii. Boti zinatumika kubeba watalii,” alisema
Mgeni alisema,”Kwa Kanda ya Ziwa Benki italeta mikopo ya boti za uvuvi, lakini endapo kuna mahitaji pia ya boti za utalii NMB itaweza kufanya hivyo.”
Alisema rasilimali na mtaji wa Benki vinakua kila mwaka kiasi kwamba sasa ina uwezo wa kukopesha hadi kiasi cha Sh.250 billioni kwa mtu mmoja.
Kwa mujibu wa Mgeni, kwa sasa rasilimali za Benki ni Sh. Trillioni 8.7 na Amana za watejaj Sh.trillioni 6.6.
Washiriki wa mkutano huo, akiwemo Mshauri wa Masuala ya Kodi katika Kampuni ya Onduchi Associate, Nicas Nibengo, alichangia akisema wafanyabiashara wote wanafahamu kwamba kulipa kodi bila shuruti ni wajibu wao, lakini serikali iendelee kuweka mazingira rafiki.
Alishauri kushuka kwa kiwango cha kodi ya ongezeko la thamani (VAT), kutoka asilimia 18 za sasa hadi 15, kama ilivyo kwa nchi ya Kenya, ili wawekezaji wa Tanzania waweze kuhilili ushindani katika sekta ya biashara.
“Kwa sasa mshindani wetu mkubwa ni Kenya. Kiwango cha VAT nchini Uganda ambacho ni asilimia 16 hakitusumbui sana,” alisema.
Alitoa pongezi kwa muandaaji wa mkutano huo ambao ulitoa fursa kwa wafanyabiashara hao kujifunza mambo mengi kwa ustawi wa biashara zao, ikiwemo utoaji mikopo ya vifaa vya kufanyia kazi, utunzaji kumbukumbu za biashara pamoja na ulipaji bora wa kodi.
Akifungua mkutano huo, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza (RC), Mhandisi Robert Gabriel, aliwakaribisha wafanyabiashara hao kuwekeza hasa katika sekta ya utalii, uvuvi na kilimo, akasema:
“Tayari serikali imeandaa maeeno ya ufugaji wa samaki wa vizimba katika Ziwa Victoria na miundombinu yote muhimu imeshawekwa.
“Tunasubiri wawekezaji tu. Lakini pia tunaweza kuwekeza kwenye kilimo cha kimkakati kwani ardhi ya Mwanza inastawisha kila aina ya mazao,” alisema na kuongeza kwamba:
Kilimo cha umwagiliaji kinawezekana kutokana na uwepo wa Ziwa Victoria ambalo maji yake niya uhakika wakati wote.
Eneo lingiine ni fukwe zilizopo kandokanod ya Ziwa Victoria kwa ajili ya ujenzi wa Hoteli kubwa za kitalii, alisema RC.
Leave a comment